Saturday, April 14, 2007

SHULE ZIWE VITUVO VYA MAENDELEO

Mwaka huu sote tumeshuhudia ujenzi wa shule nyingi za SEKONDARI. Shule zimejengwa kwa AGIZO na kweli AGIZO limefanyiwa kazi. Na sasa Wilaya zinashindana na mikoa nayo inashindana kwa kujenga shule nyingi watoto wetu wengi wamepata nafasi ya kujiunga na shule za sekondari. Hilo ni jambo zuri. Ingawa baadhi yetu wanahoji kama kweli kujenga shule ndiyo kuwa na ubora wa Elimu? Sasa baada ya shule kujengwa tuzipatie vitendea kazi na tufuatilie kuona elimu bora inatolewa

Wazo langu la leo ni kwamba hizi shule za Sekondari zinazojengwa katika kila Kata ziwe chachu za maendeleo katika nchi yetu. Sekta zote zijikite katika Kata ziliko shule kwa ajili ya kutoa huduma na kujenga uchumi. Kwa kuwa naamini kuwa kwenye shule hizo kuna watu wa aina mbalimbali ambao wasingependa kuona kuwa wametupwa. Kwa mfano hakuna mwalimu yeyote ambaye angependa kufundisha na kuishi sehemu ambayo maji, usafiri, umeme, mawasiliano ni shida. Asingependa kuishi sehemu ambayo upatikanaji wa chakula ni shida, asingependa kuishi sehemu ambayo hakuna huduma ya afya.

Kama sekta zote zitajikita ziliko shule za sekondari ni rahisi kupanga mipango ya maendeleo yenye upeo mpana zaidi na itakuwa ni rahisi kufuatilia na kupima maendeleo. Watu watajifunza kutoka kwa wengine na maendeleo yataonekana. Haya ni maoni yangu.

Nakumbuka nilipokuwa mdogo sehemu zote zilizokuwa na "Middle Schools" huduma muhimu zilipatikana. Waalimu walionekana wamaana sana, waliheshimika na walikuwa na uwezo mzuri kimaisha. Ilikuwa ni sifa kuitwa mtoto wa mwalimu kwa sababu alikuwa ni kioo cha maisha mahali pale. Sasa je? TUFUFUE MTAZAMO HUO. TUZIFUATE SHULE ZA SEKONDARI KWA MAENDELEO.

"ZOGOWALE" WANAUME WANAFANYA KAZI MASAA 4

Hivi tumeshawahi kujipima katika jamii zetu katika utendaji kazi kati ya wanawake na wanaume?

Ili kuweza kufahamu ni akina nani hasa wanaotumia muda mwingi wa kufanya kazi?Hivi karibuni kikundi cha watafiti 10 kutoka Wizara ya Kilimo Chakula na Ushirika kilisafiri hadi kijiji/mtaa wa Zogowale, Wilaya ya Kibaha, Mkoa wa Pwani ili kuweza kujifunza masuala ya Jinsia katika kijiji hicho.

Watafiti hao walifanya majadiliano na wakazi wa mtaa huu wapatao 47. Baada ya kudodosana kwa takribani masaa mawili. Iligundulika kuwa, wanaume hutumia masaa manne kwa siku kwa kufanya kazi, wakati wanawake wao hutumia masaa 12! Eeh jamani tutafika kweli? Maendeleo yatapatikanaje kwa kufanya kazi kwa muda mchache namna hiyo na huku mwanamke akiachiwa shughuli nyingi za kufanya.Hata hivyo katika utafiti huo, ilibainika kuwa, jamii ya

Zogowale imeshaanza kubadilika, kwani kwa sasa zile ndoa changa zimeanza kusaidiana katika kufanya kazi. Wanaume huchota maji, hufua nguo na hata kupika chakula! Safi sana.Je, akina baba wanawapeleka watoto wao hospitali mara wanapougua ?(yaani kuwabeba kama wanavyofanya akina mama?). Akina baba wa Zogowale bado ni wazito kwa hilo. Wao hutoa amri tu na kutoa fedha za tiba, lakini si rahisi kumkuta baba kutoka Zogowale amebeba mtoto na kumpeleka hospitali!Kumenya mihogo je? Kazi hii nayo hufanywa na akina mama. Ni mara chache sana kukuta baba akimenya mihogo.

Zogowale, maisha huanza mapema, katika umri wa miaka 20 ni rahisi sana kumkuta kijana akiishi na mwanamke na pengine kuwa na mtoto hata mmoja!
Labels: John Banzi

Wanawake wapewe kipaumbele katika kutoa mikopo

Takribani miezi miwili sasa nimekuwa nikifuatilia kwa jinsi wanawake wa Tanzania wanavyojishughulisha katika kujipatia riziki.

Kwa mfano Jijini Dar Es Salaam baadhi ya akina mama ndiyo wanaolisha wafanyakazi wa jiji hili. Si mara moja ama mbili mimi mwenyewe nilipata msosi pale Tazara karibu na Redio Tanzania kwa akina mama hao. Wanawake wanaoendesha biashara ya mama lishe wengi wao ni vijana kati ya umri wa miaka 20-45 hivi.

Kuna hii biashara ya kuuza chupa za plastic jijini Dar. Akina mama wamo, shughuli hii hapa jijini hufanywa na wanawake wa umri mkubwa kati ya miaka 40-50. Pengine vijana wanaona aibu kupita mitaani kuokota chupa ndiyo maana hawaonekani sana kwenye biashara hiyo.Pengine huokota usiku! Lakini utazionaje chupa usiku? Wazee hawaoni haya wanachotaka ni riziki. Na ikumbukwe kuwa hawa wanabeba mzigo mkubwa katika kaya wengine huishi hata na wajukuu na watoto wa ndugu zao kwa hiyo la msingi wao ni kupata riziki. Aibu ya nini?

Pale Mbagala Rangi 3 ifikapo jioni kuanzia saa 12 biashara mbalimbali huanza kufanyika. Wapo wauza matunda na mbogamboga, wapo wauza mihogo, wapo wauza korosho n.k. Lakini wanaofanya biashara hizo wengi ni wanawake wa rika mbalimbali.

Nilipokuwa kwenye semina mjini Morogoro hivi karibuni niliwakuta wanawake wakiuza nguo za aina mbalimbali kando ya kumbi za mikutano. Na si mara moja kuwaona wanawake wakifanya biashara hizo kwenye kumbi mbalimbali za mikutano. Wapo Morogoro Hotel, wapo SUA, wapo Islamic University n.k.

Baada ya kufuatilia na kudadisi sana na kuangalia ile mikopo ya bilioni moja iliyotolewa kwa kila mkoa kwa ajili ya ujasiliamali. Napenda kushauri kuwa mikopo hiyo kipaumbele wapewe wanawake. Wanawake ni nguzo ya familia kwa kweli. Wanawake wakijikwamua kiuchumi maendeleo yatapatikana kwani waathirika wakubwa kiuchumi kwenye jamii zetu ni wanawake. Lakini jitahada zao kujikwamua kiuchumi zinaonekana. TUANZE SASA