Wednesday, March 25, 2009

Kwa Joseph ni zaidi ya Ubwabwa


Watoto hupenda kula wali au ubwabwa. Hata sisi tulipokuwa watoto na hata leo bado tunapenda kula wali. Tulipokuwa tukisoma sekondari siku ya kula wali kila mmoja alikuwa msafi kwenda bwaloni. Na mgawaji alikuwa anapiga nyengo kwa wengine na kujipendelea mwenyewe kwa kujaza sahani yake. Kweli wali ni mtamu hasa na maharage. Ni chakula kinachopendwa na wengi hasa hapa Tanzania. Pichani uncle Joseph Julius akibugia ubwabwa kwa jazba!

Friday, March 20, 2009

Si nzuri sana


Hii ndiyo Uhuru PARK ya jijini Nairobi. Si nzuri sana. Tukijizatiti hii ya kwetu ya Mnazi mmoja inaweza kuwa bomba ile mbaya. Jiji anzeni kazi basi

Green House ya Kabete


Utafiti wa mahindi unaendelea ndani ya Green House ya Kabete, Nairobi Kenya.

Utapenda ule!


Hii ni sehemu mojawapo ya kupata msosi kwenye hotel Continental jijini Nairobi. Check upangaji wa matunda utapenda ule!

Twin Towers kwa mbali!


Hayo ndiyo majengo ya BoT yanayopigiwa kelele kwamba yamejengwa kifisadi. Majengo ni mazuri lakini fedha zilizotumika zinaendana na hali halisi? Ndo maana kuna badhi ya wafanyakazi waliohusika katika mchakato wa ujenzi wa jengo hilo wanatuhumiwa kwa ufisadi kesi iko mahakamani.

Kabete-Maabara Kuu ya Utafiti wa Kilimo Kenya


Hiyo ndiyo maabara kuu ya Utafiti iliyoko nchini Kenya chini ya Kenya Agricultural Research Institute (KARI) ipo Kabete- km zipatazo 10 kutoka mjini Nairobi. Hapa kuna aina zote za maabara-Biotechnology, Animal Diseases, Soil and Plant laboratories. Hapa kuna wataalamu na vifaa. Kweli pametulia.
Wataalamu wa Kutathmini na Kupelemba shughuli za Utafiti wa Kilimo kutoka Afrika ya Mashariki na Kati walitembelea kituo hicho mwanzoni mwa mwezi Machi 2009.

Yanangoja kulazwa pale Msikitini-Kilwa Road


Barabara ya Kilwa kutoka Mtoni Mtongani hadi Mbagala rangi 3 imekamilika kwa asilimia 95. Bado mambo madogo madogo tu kama hili la kulaza maculverts. Vinginevyo sasa wanambagala wanajidai kifua mbele kuwa wanakaa mjini Mbagala!

Wengi tulinyonya vidole


Wengi wetu tulipokuwa wadogo tulikuwa na tabia ya kunyonya vidole! Uncle Magge Julius akinyonya dole. Hii ni moja ya hatua za makuzi za watoto akikua ataacha. Itakuwa hadithi tu. Mage alikuwa akinyonya vidole.

Wabunge wanawake wa kesho kutoka Kisemvule


Hawa ndiyo wabunge wa kesho kutoka Kisemvule wilaya ya Mkuranga

Friday, March 13, 2009

Kushambuliwa kwa Mwinyi ni somo

Tujiulize tulikuwa wapi hadi Rais Mstaafu Alhaj Ali Hassan Mwinyi anashambuliwa jukwaani. Kama tulikuwa tunampenda mzee "Ruksa" kwanini tusimlinde? Si kila mtu anapendwa na wote. Tukumbuke binadamu tu tofauti. Tusiwaamini binadamu. Tukumbuke kuwa yule mwandishi aliyemrushia G.Bush viatu alikosa nafasi ya kumshambulia kwa karibu. Kama angepata nafasi hiyo ilivyotokea kwa Mwinyi Bush angetoweka! Hili ni somo.

Samaki hawa wangeweza kujenga sekondari

Hadi jana zaidi ya tani 90 za samaki zilikuwa zimeshapakuliwa kutoka kwenye meli iliyokamatwa ikivua samaki katika bahari ya Hindi eneo la Tanzania. Katika taarifa ya habari iliyorushwa na TBC 1 ilieleza kuwa inakisiwa kuwa inawezekana kuwa bado kuna tani 90 na zaidi. Wamekuta pia mayai ya papa na mashavu yake ambayo yana thamani kubwa huko Asia.

Ina maana miaka zaidi ya arobaini tulikuwa tunaibiwa hivi hivi. Huku tukiendelea kuwa masikini. Samaki peke yake wangeweza kujenga shule za msingi na sekondari zilizo bora na kuongeza maslahi ya walimu. Hivi miaka yote hiyo hatukujua kuwa tunaibiwa? au kuna wenzetu walikuwa wanakula nao? Hii ni zaidi ya EPA. Hongera Magufuli umepanda chati haraka sana kwa hili.

Precision Air wameweza

Hakuna ubabaishaji, uswahili na nini sijui. Precision Air inafanya vitu vya uhakika. Tarehe 1/3/2009 nilisafiri kwenda Nairobi Kenya na kurudi tarehe 7/3/2009 kwa kutumia Precision Air. Tuliondoka kwa wakati muafaka na tulirudi kwa wakati muafaka. Huwezi kuamini tulifika Dar saa 8.00 kama ilivyoandikwa kwenye tiketi huduma ndani ya ndege safi kabisa lugha nzuri na vijana wachangamfu. Kampuni hii ya ndege ni kioo bora cha nchi yetu katika usafiri wa anga ipewe ushirikiano unaostahili. Jamani Precision Air siyo tu wanaweza, wameweza.

Chonde tusiruhusu watu binafsi kumiliki ardhi "for good"


Nchi jirani wanalia kwa sera za kumilikisha ardhi watu binafsi. Ikiwemo jirani zetu wa Kenya. Tatizo la ardhi nchini Kenya ni kubwa sana kuliko wengi tunavyofikiri. Wenyewe wanasema ndicho chanzo cha migogoro isiyokuwa na mwisho nchini Kenya. Nawaoma tusimilikishe ardhi kwa watu binafsi 'for good' tutajuta. Sera yetu kuhusu umilikaji wa ardhi bado ni nzuri tuirekebishe kama kuna dosari ndogondogo.

KILWA ROAD UPDATE 7!

Mambo waa Mbagala. Wanateleza, oh tunateleza! Hivi ndivyo mambo ya livyo kwa wanaotumia barabra ya Kilwa. Kimsingi barabara imemalizika kuwekwa lami.Kilichabakia ni mifereji na nakshi nakshi tu. Mbagala TAZARA dak.23 tu.Leo nimefika saa 1.05 ofisini kutoka Kisemvule km 27 toka TAZARA!

Thursday, March 5, 2009

Kenya wanawekeza kwenye Utafiti

Leo mchana mimi na wenzangu tunaoshiriki warsha ya kupelemba na kutathmini (M&E) hapa Nairobi tumepata bahati ya kutembelea moja ya kituo cha Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Kenya (KARI) kinachoitwa NARI-Kabete. Kituo hiki kiko umbali wa kilometa 10 kutoka mjini Nairobi.
Unapoingia kwenye mazingira ya kituo hicho utapata jawabu kuwa hicho ni kituo cha Utafiti kina maabara mengi na vifaa vya kutosha. Hapa shughuli kubwa zinazofanyika ni utafiti wa udongo, magonjwa, Bioteknolojia na utafiti wa sayansi jamii (socio-economic research).

Tulipokuwa tunatembezwa kwenye moja ya screen house makubwa ya kuvutia ya kiutafiti tulijionea na kuelezwa na watafiti wa Kenya. Tunaambiwa kuwa hii ni screen house kubwa barani afrika. Watafiti wa Kenya wamepiga hatua kubwa kwenye nyanja ya biotekenolojia. Wana facility za kutosha pamoja na watafiti waliobobea. Kuna haja ya kujifunza kutoka kwao.

Wednesday, March 4, 2009

Kuna hatari ya kununua chakula kingi zaidi ifikapo mwaka 2030


Si ramli. Lakini takwimu zilizopo zinaonyesha kuwa Afrika kusini mwa jangwa la sahara inahatari ya kununua zaidi chakula ifikapo mwaka 2030 kuliko sehemu nyingine ya dunia. Lakini tujiulize. Iwapo kila sehemu kuna matatizo ya chakula nani atamuuzia mwenzie. Na hata hivyo, je uwezo wa kununua chakula hicho kitatatoka wapi? Tanzania tupo wapi? Tufikiri na kufanyia kazi takwimu hizi.Si ramli ni ukweli mtupu. Pengine wengi wetu tutakuwa hatupo duniani.Lakini tusije kulaumiwa na watoto au wajukuu wetu.

Tanzania inayo nafasi nzuri ya kuzalisha mpunga


Hali ya uzalishaji wa mazao ya nafaka duniani kwa sasa si nzuri.Uzalishaji umeshuka sana na bei ya mazao ya nafaka kwa nchi nyingi duniani inazidi kupanda.


Mwenendo huu ingawa siyo mzuri, lakini unaipa nafasi Tanzania kuzalisha zaidi mazao ya nafaka kwani soko lipo. Moja ya mazao ambayo Tanzania tunaweza kuzalisha kwa wingi na kuweza kujitosheleza kwa chakula na kuweza kupata soko nchi nyingine ni zao la mpunga.


Tanzania tuna ardhi ya kutosha, vyanzo vingi vya maji na hata utaalamu upo. Kinachotakiwa ni juhudi za kusudi ili kuweza kutumia fursa iliyopo. Watanzania tubadilike fursa zipo tuzitumie. Wenzetu k.m.Amerika asilimia 5% ya wananchi wanaojishughulisha na kilimo wanalisha asilimia 95% na kuuza ziada. Tanzania asilimia 85 ni wakulima lakini wanashindwa kulisha asilimia 15 ambayo haijishughulishi na kilimo? Kwa mwenendo huu hatuwezi kuendelea hata kidogo.

Tusipokuwa makini hata ziwa Victoria litapotea

Tusifikiri utani tunapoambiwa kuwa tusikate miti. Tutunze mazingira.Watu wengine wanafikiri ni masihara. Tusipokuwa makini hata ziwa Victoria linaweza kupotea!

Leo mchana Mkurugenzi Mtendaji wa ASARECA Dr.S.Ketema aliwasilisha mada ambayo ilivutia sana wakati mwingine iliniweka katika fikra nzito na tafakari ya kina yenye kukata tamaa lakini wakati mwingine kuwa na matumaini iwapo tutapambana haraka kunusuru hali ya sasa. Hii yote inatokana na hali halisi ilivyo katika ulimwengu huu tunaoishi.

Moja ya mfano hai alioutoa ni ziwa lilikuwepo Ethiopia miaka 20 iliyopita sasa limekauka kabisa kiasi cha kufanya watu waanze kulima kwenye eneo lote lililokuwemo ziwa. Hii yote ni kutokana na kutokuwa makini katika utunzaji wa mazingira.Watu wamekata miti ovyo kwa muda mrefu na hivyo kuathiri mazingira yanayolizunguka ziwa hilo.Tatizo si kukauka kwa ziwa tu bali ni jinsi uzalishaji unavyoathirika na hatimaye kuathiri maisha ya watu.

Tuesday, March 3, 2009

Ni vizuri wakulima wanapotumia teknolojia bora

Wengi hatujafahamu umuhimu wa utafiti. Na kwanini serikali inabidi kuwekeza kwenye utafiti. Bila utafiti katika sekta yoyote hatuwezi kuboresha uzalishaji au huduma. Utafiti unahitajiwa kwenye afya, kilimo, elimu,viwanda, biashara na huduma nyinginezo.


Watafiti wanafarijika sana wanapoona kuwa teknolojia au uvumbuzi wao unatumika. Pichani mkulima akipanda mbegu bora za mahindi zilizofanyiwa utafiti.

PRRR.. KUMBE NI MKENYA

Jana nilikuwa nikiangalia kipindi kimoja cha mahojiano katika NTV hapa Nairobi. Ni mahojiano na moja wa magwiji wa sanaa nchini maarufu kwa jina la "papa shilandula" baadaye nilikuja kugundua kuwa huyu ndiye aliyeshiriki kwenye tangazo la cocacola la PRRR linaloonyeshwa kwenye TV.

Msanii huyu kwa kweli ana kipaji. Kwanza anaongea kwa mantiki anajua anachokifanya na anategemea nini. Nilichojifunza kwake ni kuwa hana makeke. Hata gari lake ni la kawaida kabisa. Ni kipande cha baba kweli. Hata kiingereza chake ni safi sana. Mahojiano yale yalikuwa mazuri sana. Wasanii wetu wanaweza kujifunza kutoka kwa "papa shilandula" (jina la kisanii).

Kilimo bora ni pamoja na usafiri wa uhakika


Tunapozungumzia kilimo bora si mbolea pekee wala si maji pekee wala si mbegu tu na pengine si matrekta. Kilimo bora ni pamoja na kuwa na usafiri wa kusafirisha mazao kutoka shambani hadi ghalani, kiwandani au sokoni.


Zao la chai ni moja ya zao linalohitaji usafiri wa uhakika na wa haraka mara tu chai inapovunwa kutoka shambani kwenda kiwandani ili itayarishwe kuwa majani ya chai. Bila ya kuwa na usafiri wa uhakika chai huharibika. Hii huwa ni hasara kwa mkulima. Kwani chai ya mkulima inakuwa na thamani inapofika kiwandani kwa wakati. Hivyo basi ni muhimu wakati tunapozungumzia kilimo tuwe na muono mpana. Pichani wakulima wakipakia chai katika lori maalumu lilitengenezwa kusoma chai kutoka mashambani.

Mfumo wa Kupelemba na Kutathmini uwe na meno


Wataalamu wa Kupelemba na Kutathmini wanaoendelea na warsha iliyoandaliwa na ASARECA hapa Nairobi Kenya katika mada zao wamesisitiza kuwa wakati umefika wa kuweka mfumo wa M&E wenye meno. Wakiwa na maana kuwa ikiwa mambo hayaendi kama yalivyopangwa katika shughuli za utafiti lazima hatua zichukuliwe. Kwa mfano hakuna sababu ya kuendelea na utafiti ambao unaonekana dhahiri kuwa hautakuwa na mafanikio.


Hakuna sababu ya kuwa tafiti mpya kila mwaka kama hakuna umuhimu wa tafiti hizo. Aidha hakuna haja ya kuwa na mtafiti mzembe! Hata hivyo wametahadharisha kuwa M&E siyo polisi. Lakini ni mfumo wa kutoa ushauri ya nini kifanyike ili kilete mafanikio yaliyokusudiwa.

Nipo Nairobi


Nipo Nairobi tangu tarehe 1 Machi 2009. Tunakutana na watafiti wenzetu kutoka nchi zilizo katika umoja wa ASARECA wanaojishughulisha katika masuala ya Kupelemba na Kutathmini (Monitoring and Evaluation) shughuli za Utafiti na Asasi zake. Wawakilishi kutoka vyuo vikuu kama vile Eagarton wapo pia. Burundi, Rwanda na Madagascar wameleta wawakilishi wao pia ingawa wanaongea Kifaransa lakini wapo hapa na tunawasiliana kwa kiingereza. Yatakayojiri nitayaning'iniza kwenye blog hii. Kwani siyo siri. Ni warsha ya majadiliano, kuongeza maarifa na kupanga mipango ya nini kifanyike katika kuimarisha vitengo vya M&E katika Asasi zetu za Utafiti.Lengo ni kuboresha shughuli za utafiti ili kuongeza uzalishaji katika sekta ya kilimo na kuinua maisha ya wakulima wetu.

Monday, March 2, 2009

Iwapo tutakwepa kodi nchi haiwezi kuendelea


Watanzania wengi hawalipi kodi.Hawaoni umuhimu wa kulipa kodi lakini wanataka maendeleo. Wanalamikia kiwango duni cha elimu, huduma duni ya afya, barabara mbovu, haduma za umeme na maji zisizo ridhisha. Hii ni mifano tu ya huduma zinazoweza kuboreshwa iwapo kodi zinazohusika zitalipwa.Tukilipa kodi serikali inaweza kuaagiza matrekata madogo (pichani) yatakayowarahisishia wakulima wetu shughuli za shamba.

Tunanunua vitu madukani lakini hatupewi stakabadhi.Wafanyabiashara wengi wanakwepa kodi tena za mabilioni. Kwa mwendo huu tutaweza kuwalipa walimu wetu mishahara mizuri, madaktari wetu na wafanyakazi wengine. Watanzania wenzangu tulipe kodi kwa maendeleo yetu na maisha bora.