Thursday, December 31, 2009

KWAHERI 2009 KARIBU 2010

Pamoja na changamoto nyingi zilizojitokeza kwa mwaka 2009. Namshukuru Mungu mwaka 2009 ulikuwa wa mafanikio kwangu. Nawashukuru wote walionisadia kufikia malengo yangu. Nawashukuru wote waliopata fursa ya kupitia blog hii. Shukurani za pekee zimwendee Prosper Bello aliyekuwa wa kwanza kufuatilia blog hii na kutoa maoni yake. Namshukuru pia mfuatiliaji wa pili aliyejitokeza mwaka huu ambaye ameonekana kuwa mfuatiliaji mzuri wa Banzi wa Moro (Haja taja jina). Ingawa nimeshindwa kufikia lengo la kuning'iniza vitu 365 lakini 250 nazo si haba nimevunja rekodi ya mwaka jana. Endapo Mungu akinijalia nikaweza kumiliki camera yangu mwenyewe naahidi kuwaletea vitu vizuri mwaka 2010. HAPPY NEW YEAR.

NAMSHUKURU MUNGU NIMEWEZA KUNING'INIZA MENGI KWENYE BANZI WA MORO


Pamoja na majukumu mengi na mapya niliyokuwa nayo mwaka 2009 lakini namshukuru Mungu nimeweza kuning'iniza mengi katika blog hii. Kuna wakati nilining'iniza chache sana hasa mwezi Novemba 7 tu. Sababu ni nyingi- mtandao kugoma, na kutingwa na shughuli za ofisi pamoja na misiba haya yalionifanya nishindwe kutuma mambo mtandaoni. Namshukuru Mungu

MWAKA 2009 NILIIKOSA XMASS YA MATOMBO

Nilipanga kwenda kijijini Matombo Morogoro kwa likizo ya muda mfupi kusherekea sikukuu ya XMASS mwaka huu ilishindikana kutokana na majukumu ya hapa kazini. Pengine hiki ni moja ya kitu nilichokikosa mwaka huu

Kila kifo ni cha ghafula-Sheikh Yahya

Mapema leo asubuhi nilikuwa nikitazama kipindi cha Jambo Tanzania kinachorushwa na TBC. Mmoja wa wageni waliokaribishwa katika kipindi hicho ni Mnajimu wa siku nyingi Afrika Mashariki na Kati Sheikh Yahya ambaye hivi karibuni utabiri wake uliodai kuwa atakayegombea nafasi ya Rais katika uchaguzi wa mwakani kumpinga Rais wa sasa Mhe. Jakaya Kikwete atakufa ghafla. Akionyesha uhodari wa kujenga na kutetea utabiri wake na hoja hiyo alisema kuwa wanadamu tusiogope kifo kwani kinapotokea kina faida na hasara. Kwa mfano ni pale tu mzazi anapofariki ndipo watoto wanapopata fursa ya kurithi mali za mzazi.

Samaki mkunje angali mbichi


Ni dhahiri mtoto huyu akiendelea kushirikishwa kazi za shamba na kukipenda kilimo tangu utoto wake hatochukia kilimo na hatochukia maisha ya shamba. Samaki mkunje angali mbichi.

TUTOKE HUKU


Vijiji vingi vya kiafrika haya ndiyo maisha ya wakulima.Usafiri wa shida, nyumba duni miundo mbinu ya kubahatisha. Lakini hebu angalia kwenye picha unavutiwa na rangi ya kijani ya uoto. Maana yake rutuba ipo. Je, wakulima wetu wataendelea kuishi kwenye mazingira haya mpaka lini? Hata, tutoke huku.

Simu inapotumika na mkulima kutika kupanga bei ya mazao shambani


Mwisho huu wa mwaka nawaletea picha iliyoshinda kwenye mashindano yaliyoendeshwa na jarida la kimataifa liitwalo 'Farming Matters.' Picha hii ni ya wakulima wa Phillipines maarufu kwa zao la mpunga. Mkulima anaweza kuwasiliana na mfanyabiashara kwa kutumia simu ya kiganjani kabla ya mavuno hivyo kuepukana na walanguzi kwani kwa kupitia simu majadiliano kuhusu bei hufanyika.

KAWAWA AMETUACHA


Simba wa Vita na mkongwe wa Siasa katika Historia ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rashidi Mfaume Kawawa amefariki leo asubuhi. MUNGU ailaze mahali pema peponi roho ya Mzee wetu, Kiongozi wetu asiye na makuu Marehemu Kawawa.

Tuesday, December 29, 2009

Mifereji ya barabara ya Kilwa isilipuliwe

Kuna zoezi linalokwenda kwa kasi la kujenga mifereji kwenye barabara ya Kilwa. Naambiwa kuwa hilo lilikuwa ni agizo la Mhe. Waziri Mkuu, Mizengo Pinda aliyeagiza mamlaka husika kushughulikia mifereji hiyo haraka iwezekanavyo kuepusha hatari ya kuharibika barabara mpya iliyojengwa. Ninachoona mimi ni kuwa mifereji hiyo inajengwa haraka lakini si kwa kiwango kinachotakiwa. Ni kweli wajenzi ni wazawa. Lakini uzawa isiwe 'issue' ya kulipua kazi. Kwa maana nimeshaona baadhi ya maeneo mifereji imeshaanza kuchimbika kutokana na mvua hizi zinazonyeesha.

Dawasco bomba linavuja kituo cha Msikiti-Kilwa Road

Leo asubuhi wakati nikija kazini karibu kabisa ya kituo cha Msikiti mara baada ya kumaliza makaburi ya Mbagala Mission tulikuta maji ya kitiririka barabarani yakiashiria kuvuja kwa bomba. Hatari ni kwamba hali hiyo isipodhibitiwa haraka maji yatachimba barabara na hivyo magari kukwepa shimo hilo hatimaye kusababisha msongamano wa magari pengine hata ajali ndiyo maana nawakumbusha DAWASCO wafanye hima kurekebisha hali hiyo.

Garage za mtaa wa Mkumba-Wailes ni uchafu

Jana jioni wakati nikitoka kazini nilibahatika kupitia mtaa wa Mkumba uliopo Wailes-Temeke na kuona magari mabovu pande zote za barabara hiyo. Nilipojaribu kuuliza ni kwanini kuwepo kwa hali hiyo? Nikajibiwa aah mzee usishangae hizo ni garage za mitaani.

Hivi kweli watendaji wa Temeke mmerizika na hali hiyo? Jiji hili bado kunakuwa na garage za mitaani? Aah ondoeni uchafu huo haipendezi hata kidogo.

Monday, December 28, 2009

Yanga Imara bado


Gazeti la Yanga Imara halivutii hata kidogo. Ubora wa gazeti hili kuanzia karatasi zake, usanifu pamoja na habari zenyewe hazivutii hata chembe ni za kitoto mno. Hebu soma ukarasa wa mbele wa gazeti hili lililotoka leo kufuatia Yanga kutwaa ubingwa wa TUSKER CUP. Mwee kichefuchefu kabisa.

RUZUKU IPIMWE KWA UZALISHAJI


Yapata miaka mitatu sasa tangu serikali ianze utaratibu wa kutoa ruzuku ya pembejeo hasa mbolea kwa wakulima hapa nchini. Ruzuku hii hutolewa kwa mfumo wa vocha. Mfumo huu wa ruzuku kwa kutumia vocha unakuwaje hasa. Hapa kichafanyika ni kwa serikali kugharamia asilimia fulani ya gharama za pembejeo kwa mfumo wa vocha hivyo kumpunguzia makali ya uzalishaji mkulima. Mfumo huu ulipoanza ulikumbana na matatizo mengi kila mwaka maboresho yamekuwa yakifanywa ili ruzuku iweze kutoa matokeo yanayokusudiwa. Mimi naamini kuwa matokeo mazuri yatapatikana kwa kuongezeka uzalishaji na kuleta tija kwa wakulima.

SIKUKUU NI YA WATOTO


Hivi ndivyo ilivyokuwa kwa watoto hawa wa kijiji cha Kisemvule wilaya ya Mkuranga, Pwani walivyosherehekea sikukuu ya X-mass 2009. Wameulamba na kwa kweli wamependeza. Watoto walipiga picha hii baada ya kupata pilau nzito. Baadaye wakatafuna korosho na embe hii ndiyo raha ya pwani usipime mwanangu!

Friday, December 18, 2009

Ni kweli mazingira ya dhiki hayatakuza elimu


Wakati nakaribia kutoka ofisini siku ya Ijumaa. Kwa haraka nilipata kusoma kichwa cha habari kisemacho "Mazingira ya dhiki hayatakuza elimu" makala iliyoandikwa kwenye gazeti la Rai 17-23 2009. Kichwa cha habari hii kimenivutia kusoma makala hii iliyoandikwa na Masumbuko Nesphory. Serikali haitaki lawama na walimu nao hawataki kulaumiwa. "Tuache siasa tuache porojo katika elimu. Tusilaumiane tuwajibike." Anamaliza mwandishi wa makala hii. Mwandishi ameandika mengi kwa pande zote mbili. Ni kweli mazingira ya sasa ya kutoa elimu kwa shule za umma hayaridhishi. Tafuta gazeti hili na soma makala hiyo. Picha kushoto kwa hisani ya gazeti la Rai

Naambiwa hiki ni kijiji cha China


Miaka takribani ishirini iliyopita China ilikuwa ikidharaulika sana. Labda ilikuwa ikiogopwa kwa wingi wa watu wake na umahiri wao kwenye vita. Lakini nchi za magharibi iliiponda sana hasa kutokana na siasa yake Ujamaa.

Lakini sasa ni tishio. Waamerika wanaigwaya China. Kitu gani ambacho China hawawezi kukifanya. China wamebakia kuwa wajamaa huku wakiboresha maisha ya wananchi wao. Hebu angalia picha kushoto kwako, hicho ni kijiji mojawapo kilichopo China. Wanapanga na kutekeleza haya ndiyo maendeleo tunayotaka. Ubepari sawa lakini kwa faida ya nani? Ubepari huku tunashindwa kuzibua mitaro ya maji machafu? Ubepari huku tukishindwa kupaka rangi hata majengo ya umma?Ubepari wakati makao makuu ya nchi umeme kwa mgao?

Ziara za mafunzo kwa wakulima


Moja ya urithi alioucha marehemu mama yangu ni doti ya Khanga iliyoandikwa "Tembea Uone" Ni kweli mimi mwenyewe nimetembea na kuona mengi na kujifunza mengi na kuacha mengi.

Tunapotaka wakulima wajifunze teknolojia mpya moja ya mbinu zinazotumika ni kuwapatia ziara za mafunzo. Bado tunaamini kuwa "Tembea uone." Kwenye ziara hizi wakulima huona na kujifunza haraka. Wanaweza kujifunza jinsi ya kufuga kuku kutoka kwa wakulima wenzao kwa mazingira yanayofanana na ya kwao, jinsi ya kulima aina fulani ya zao kama vile nyanya, vitunguu n.k. kwa ufanisi zaidi. Wanajifunza pia jinsi wakulima wanavyoweza kujenga nyumba nzuri kwa kutumia raslimali walizonazo. Wanaweza kujifunza pia kumbe hata mkulima wa embe anaweza kumiliki gari!
Ukiona huwezi kusahau kwa urahisi. Nahitimisha kwa kusema kuwa ziara za mafunzo kwa wakulima ni muhimu. Pichani wakulima wakiwa katika ziara ya mafunzo wakionyeshwa namna ya kuchota maji kwa ajili ya umwagiliaji toka kwenye kisima nyumbani kwake huko Ibumila Njombe.

Ungefuga kuku wa kienyeji


Sikukuu ya X-MASS na mwaka mpya inakaribia. Ni wazi kuwa bei ya nyama itaongezeka hata mara mbili. Familia nyingi hazitoweza kumudu kula nyama. Nyama ya kuku ndo usiombe kabisa nafikiri X-mass hii kuku atauzwa kuanzia shilingi 10,000 hadi 20,000/- Lakini mwananchi naomba nikuulize utashindwa kweli kufuga kuku wawili au watatu kwenye kibanda kidogo kwa mfumon huria? Mimi naamini ungefuga kuku wa kienyeji usingetaabika na kitoweo wakati wa sherehe hizi zinazokaribia tubadilike tuanze kufuga sasa kwa ajili ya Pasaka na Idd-Elftri ya mwakani.

Tuwasikilize wakulima kuhusu mfumo wa stakabadhi ghalani


Nimewasikia wakulima wakilalamika kuhusu mfumo wa kuuza mazao wa stakabadhi ghalani. Pengine wazo ni zuri lakini utaratibu uliopo wa kuwezesha mfumo huo kufanya kazi haujakaa sawa. Nikiwa kwenye gari dogo la abiria likitokea Mkuranga kwenda Mbagala Rangi tatu mama mmoja alikuwa akiulalamikia mfumo huo kwa zao la korosho. Fedha wanazolipwa mara tu wanapouza korosho ni kidogo aidha malipo yaliyosalia hayajulikani yatalipwa lini. Kwa maoni yake anaona heri korosho zao zingenunuliwa na wafanyabiashara wa kujitegemea kuliko vyama vya ushirika. Kwa hili tuwasikilize wakulima na penye dosari turekebishe.

TUSIDHARAU KAULI WANAZOTOA VIONGOZI WA DINI


Hivi karibuni gazeti moja litolewalo kila siku hapa nchini liliandika kuwa "KILIMO KWANZA NI WIMBO TU" kauli hii imetolewa na Mhashamu Kardinali Polycarp Pengo kiongozi wa Wakatoliki hapa nchini.

Tulio wataalamu wa Kilimo tusibeze kauli hii eti kwa kuwa sisi na watu wa kilimo au kuona kuwa Pengo hakipi umuhimu KILIMO. Viongozi nan wataalamu tujiulize kipi kifanyike ili kweli KILIMO KIONEKANE KUWA KWANZA hapa nchini. Tuone mabadiliko kwenye sekta hiyo kuanzia kwenye kupanga raslimali na utekelezaji wake vinginevyo inawezekana kabisa kuwa WIMBO TU. Kwa maoni yangu huenda viongozi wa dini wako sahihi. Hawa wako karibu sana na wananchi na wananchi huwa huru kueleza hisia zao kwa viongozi wa dini.

Wednesday, December 16, 2009

Kwanini Benki Kuu?


Leo hii kuna habari nyeti kwenye gazeti la Rai Mwema Desemba 16-Desemba 22,2009 inayosema "Ulaji wa Vigogo wa BoT wahojiwa." Ninachohoji mimi ni kwanini wafanyakazi wa Benki Kuu wanapewa kipaumbele katika maslahi? Mishahara yao ni ya Juu. Bado wanapewa motisha wa kukopa kiasi kikubwa cha fedha. Na inawezekana kabisa bila riba. Ikiwa mfanyakazi wa chini kiwango cha kukopa ni milioni 30 Mungu akupe nini. Kuna haja gani ya kusoma hesabu au fizikia nchi hii ikiwa kwa kuwa muhudumu wa ofisi tu Benki unalipwa mshahara mkubwa kuliko Mhandisi au Bwanashamba?

Hivi karibuni Rais Jakaya Mrisho Kikwete alitoa agizo kwa watafiti wa sekta ya kilimo kuongezewa mishahara yao kutokana na kazi nzuri wanayoifanya katika sekta hiyo. Hadi leo agizo halijatekelezwa. Kwa hali hii nani afanye kazi sekta ya kilimo. Watoto wetu watakimbilia sekta nyingine hasa za fedha. Tuangalie hili. Picha kushoto Prof.Beno Ndulu, Gavana wa Benki Kuu Tanzania.

Jamani eh Maximo kichwa ngumu tuachane naye


Karibu miaka mitano sasa. Sioni la kushangaza kutoka kwa Maximo kwa timu yetu ya Soka ya Taifa. Nionacho mimi ni kutuchanganya tu. Tunaishi kwa matumaini kuwa iko siku. Siku iko wapi wakati kila siku anaunda timu ya Taifa. Kocha mwenye kinyongo kwa baadhi ya wachezaji, kocha asiyejua lugha yetu ya Taifa kweli huyu ni kocha? Tuachane naye. Kiasi anacholipwa Maximo hata kama nusu yake angalipwa Mziray, Kibadeni, Mkwasa, au Kayuni timu ingefanya vizuri tu. Timu inapata misaad ya nguvu kutoka kwa NMB, Serengeti na wadau wengine lakini upangaji mbovu wa timu ndo unaoiua Taifa na Kilimanjaro Stars

TUACHE MALUMBANO YASIYO NA MSINGI TUJENGE NCHI

Kwa muda mrefu sasa kumekuwa na malumbano yasiyo kwisha kwa viongozi wa vyama vya siasa wakituhumiana kama watoto wadogo. Huyu akimwambia mwenzake hana elimu, mwingine akimweleza mwenzie hana busara. Na hawa wote ni watu wakubwa kwenye vyama vyao. Wakati wananchi wengine wakihangaika jinsi ya kupata riziki tena kwa shida kubwa. Wakubwa hawa wako kwenye malumbano tena kwa faida yao. Watoto wetu wanapata elimu duni, hospitali za umma bado ni dhaifu kwa huduma zinazotolewa, miundo mbinu bado ni duni. Wananchi wananyonywa vibaya kupitia simu za mkononi, miji yetu ni michafu hasa Dar.Tuache malumbano tujenge nchi yetu.

Sunday, December 13, 2009

Kutemewa mate ni dharau

Mtu anapokutumea mate ni dharau. Huyu Mkanada aliyemtemea mate askari wetu wa barabarani pamoja na mwandishi wetu wa habari Jerry Muro amefanya dharau kubwa kwa nchi hii. Kwa maoni yangu wazungu walio wengi wanatudharau sana sisi waafrika hata ukitembelea nchi zao utaona kabisa dharau machoni mwao. Kama kicheko basi ni cha kejeri. Pamoja na kuwa aliyefanya kitendo hicho ni mfanyakazi wa balozi hiyo, naomba serikali yetu iwe na msimamo kwa hili wasituchezee.

Do value chains help farmers out of poverty?


While reading a journal titled-KILIMO endelevu Africa Vol 1 issue 1 July 2009 I came across on a debate titled above-in summary the issue is- "does an emphasis on value chain development indeed lead to farmers becoming more entrepreneurial And is it the key to poverty reduction in rural areas?" Please kindly discuss. Karibuni.

Kipi kinachoitangaza Tanzania?

Elimu ya msingi, wanafunzi 50% hawakufaulu mtihani wa darasa la saba mwaka huu. Jiji la Dar Es Salaam ni chafu. Uzalishaji katika kilimo bado ni wa chini. Miundo mbinu ni ya ubabaishaji. Umeme si wa uhakika. Maji ni kwa mgao. Michezo- Mpira wa mguu timu ya Taifa haijafanikiwa kupata ushindi na kutwaa kikombe kwa muda mrefu. Madini ndo tunaambulia athari za kuharibika kwa mazingira pamojan na wananchi kupata vilema badala ya kuwa matajari. Hivi Tanzania ukiondoa amani na usalama tuna lipi la kujivunia. Hata usafi tu ni issue! Mwe!

Kuwasimamisha MAJEMBE ni kupunguza kasi ya mabadiliko

Kwa kawaida binadamu hapendi mabadiliko. Hasa mabadiliko HASI. Hivi karibuni uongozi wa JIJI la Dar Es Salaam waliamua kuwatumia MAJEMBE Auction Mart kudhibiti hali mbaya ya usafiri hapa jijini wakisaidina na Traffic Police. Zoezi hilo halikudumu kwa muda mrefu baada ya wamiliki wa mabus kutishia kugoma (hasa kwa njia ya TABATA waligoma). Hatimaye kuufanya uongozi wa mkoa wa Dar Es Salaam kusitisha zoezi hilo. Jamani tusiogope mabadiliko tuyafanyie kazi na tutazoea tu. Kwa kawaida binadamu hapendelei mabadiliko HASI.

HONGERA JKT

Kama kuna jeshi lililoonyesha ukakamavu wa hali ya juu na kushangiliwa na maelfu ya wananchi waliokuwepo uwanja wa UHURU tarehe 9 Desemba wakati wa kusherehekea miaka 48 ya UHURU ni JKT. Walipendeza kwa sare, ukakamavu na kuwajibika pamoja na kufurahisha. HONGERA SANA JKT

Mawaziri kupanda waingia uwanjani kwa mabus miaka 48 ya UHURU

Nilikuwepo uwanja wa UHURU kwenye sherehe za miaka 48 ya Uhuru. Kwanza nikiri kuwa hii ni mara yangu ya kwanza kuhudhuria sherehe za uhuru katika uwanja wa UHURU. Pamoja na viburudisho vya ngoma za kitamaduni kutoka hapa nyumbani na nchini Uganda (Kikundi cha NDERE) na gwaride la vikosi vya majeshi ya polisi,jwtz, magereza,jkt + Halaiki ya wanafunzi. Kipya ni Mawaziri, Mabalozi, Wakurugenzi kuingia uwanjani na mabus ya kukodi. Naambiwa magari yao waliyaacha KARIMJEE! Hivi hili waandishi hawakuliona?