Friday, November 23, 2007

TANESCO MPAKA MPANDISHE BEI?

Moja shirika la umma linalotoa huduma hapa Tanzania ambalo linawakera wananchi basi ni TANESCO. TANESCO haijapata kusifiwa hata mara moja. Na sikumbuki kama TANESCO imeshawahi kutangaza faida. Kila wakati wao wanajiendesha kwa hasara na kila wakati wananchi wananung'unika na huduma zao.

Kuingiza umeme ndani ya nyumba utasumbuana na TANESCO! Kulipia bills ni matatizo hasa wanaotumia mita kila wakatia mita zao zinasoma zaidi ya matumizi. Sasa wamekuja na jipya wanataka kuongeza malipo zaidi kwa kuingiza umeme ndani ya nyumba au kiwanda pamoja na malipo zaidi kwa matumizi ya umeme. Hebu tufikiri kweli mwananchi wa kawaida anaweza kulipia Tshs 500,000/= ili apate umeme nyumbani kwake. Sote tunafahamu jinsi umeme ulivyo muhimu kwa maendeleo yetu. Kwa mwendo huu wa TANESCO tutafika? TANESCO hamfanyi vizuri mapaka mpandishe bei?

NAKUFAGILIA RAIA MWEMA

Nimeshikilia gazeti jipya "Raia Mwema" Toleo Na 4. Hili ni gazeti makini linalotokana na waandishi makini waliobobea,gazeti linalotoa uchambuzi wa kina. Ndiyo maana nalifagilia. Hebu angalia makala za toleo hili- Chadema, Zitto Kabwe na hadithi ya Keki, Watu weusi tuna akili ndogo?, Ngoma inapotawaliwa na harufu mbaya,Spika Sitta na vazi lake kutoka London!Nani anayeuzima mshumaa wa Serikali? Na nyingine nyingi unaposoma unatafakari, unapata ujumbe. Hili si gazeti la utani utani, la porojo, udaku!


Asante Ulimwengu na timu yako kutuletea Raia Mwema.

VETA MTWARA BORESHENI HUDUMA!

VETA MTWARA ni moja vyuo bora hapa nchini vinavyotoa elimu ya Ufundi. Chuo hiki kimejengwa kwa kufadhiliwa na serikali ya Japan. Chuo kimejengwa kando kando ya bahari ya Hindi sehemu inayojulikana Shangani ambayo ni maarufu sana pale Mtwara.

Chuo hiki kinauwezo wa kuchukua wanafunzi wapatao 1000 kwa wakati mmoja.
VETA Mtwara pamoja na kutoa mafunzo mbalimbali pia ina vitega uchumi vingi kama huduma za malazi, chakula na kumbi za mikutano.

Pamoja na mazingira mazuri yaliyopo VETA Mtwara, huduma zitolewazo bado ni hafifu hasa kwa upande wa chakula. Wahudumu hawachangamkii wateja na unapotaka huduma unaweza kuambiwa hakuna. Chakula- Hakuna, Kinywaji - Hakuna. Eh basi kwaheri.

Kwa kweli inasikitisha wakati mwenyeji wako anapokutoa na kukupeleka mahali fulani ambapo anategemea kuwa unaweza kupata huduma safi anavunjwa moyo na hizi HAKUNA HAKUNA.

VETA Mtwara ni Taasisi ya kujivunia mjini Mtwara na sitoshangaa kama itakuwa CHUO KIKUU hapo baadaye. Lakini boresheni huduma zenu.

Tuesday, September 11, 2007

HAMKUJUA KAMA NI MHINDI?

Mengi yamesemwa kuhusu Mshindi wa Miss Tanzania wa mwaka huu. Wengine wanalalamika eti kwanini mshindi amekuwa Mhindi? Jamani, huyu Mhindi ametokea mbali katika Kinyanga'anyiro hiki nafikiri kutoka Mtaa hadi pale wilayani Kinondoni. Wakati anashinda pale Kinondoni hakuwa Mhindi? Je, Richa Aidha alipokuwa Miss Earth 2000 kule Phillipines hakuwa mhindi? Miss Indian Ocean 2006 hakuwa mhindi ?Watanzania acheni ubabaishaji.

Mimi siyo mfuatiliaji mzuri wa mashindano haya kwani nayaona ni ya kibabaishaji. Tunaigaiga tu mamabo bila kufahamu jinsi yanavyoendeshwa. Ndo maana akipatikana mshindi Mhindi tunaanza kulalamika lakini huko tunakokwenda tunawata wahindi, waingereza, warusi, wajapani sasa cha ajabu kipi. Vigezo vilivyowekwa ni vya kimataifa. Si vya Kiluguru (kucheza ngoma), Kichagga (kukatiakatia majani ng'ombe) kizaramo (shughuli)................

Kama uwezo wa Richa wa kuongea Kiingereza ni mkubwa kuliko wengine kwanini wengine wasiongea lugha wanayoifahamu vizuri (kiswahili). Sote tunafahamu tulio wengi uwezo wetu wa kuongea kiingereza ni ule wa ehe eh! You know, the, the nyingi tu. Mtu anaambiwa chagua utaongea kwa kutumia lugha gani anasema "English" haya mama twende kazini. Hata kueleza jinsi anavyoifahamu Tanzania hoi! Sasa tunalalamika nini? We Hoyce Temu mwaka 1999 ulikuwa Miss Tanzania kwenye mashindano ya Miss world hukuiona hata namba 50! Hakuna siasa hapa tupeleke wawakilishi wenye vigezo vinavyokubalika. Tikitaka dada zetu weusi washinde tuwaandee vizuri kwani huko wanakokwenda weupe ni wengi kuliko WEUSI. Hongera Richa usijali maneno ya Waswahili ndo walivyo.

NI KWELI TAIFA STARS UWEZO MDOGO

Niko na karadio kangu kadogo hapa ofisini. Mimi huwa napenda kusikiliza kipindi cha "Power Break Fast" kinachorushwa na "Clouds Radio FM." Dakika chache zilizopita Gerald Hando alikuwa anajaribu kulinganisha uwezo wa "Taifa Stars" na " The Mambas." Kwanza alisema kitimu Taifa stars ilionyesha uwezo mdogo hata wachezaji binafsi hawakuonyesha uwezo wao ukilinganisha na wenzao wa Msumbiji.

Sikwenda uwanja wa Taifa siku ya tarehe 9/8/2007. Nilibaki nyumbani nikiangalia mechi hiyo kupitia Luninga. Mchana wa siku hiyo nilibahatika kwenda Magomeni kupitia uwanja wa Taifa. Kila nilikopita nilikutana na bendara ya Taifa, saa 6 tu mchana tayari nje ya uwanja wa Taifa umati mkubwa ulikuwa umefurika wakiwa na bendera za Taifa gari zilizopambwa. Lakini cha ajabu niliiona pia pickup moja yenye mashabiki wa Timu ya Msumbiji hawakuwa wengi lakini walipendeza na walijiamini. Wakati tukilipita gari hiyo kwa mzaha sijui mmoja wao alinyoosha vidole viwili akimaanisha kuwa tutafungwa magoli mawili. Huo ulikuwa mzaha . Hata hivyo support waliyoipata timu ya Taifa katika mchezo wa Jumamosi ilikuwa kubwa sana karibu kila Mtanzania alihamasika. Hapa ninapoishi nina jirani yangu Mchaga ambaye kwa kawaida si shabiki wa soka lakini nilishangaa kumuona amefunga bendara ya Taifa kichwani. Nikamuuliza vipi Mangi au ndo umaahidiwa "pesa" akasema we acha tu, vijana lazima washinde leo!

Lile goli la dakika za mwanzo lilitumaliza Watanzania. Timu ilicheza bila uelewano. Ivo Mapunda alikuwa akibabaika. Beki inakatika. Viungo hakuna. Washambualiaji ndo kabisa kulikuwa hakuna. Unategemea nini katika hilo. Nilikuwa nasikiliza kwa makini mawaidha ya Juma Pondamali Meshah aliyokuwa akiyatoa kupitia TVT. Mara kwa mara alikuwa akisema kuwa inaonekana Ivo hana mawasiliani na beki zake. Timu inashindwa kupita katikati kwahiyo wajaribu kupitia pembeni. Kwa sababu, kipindi cha kwanza hakukuwa na "fighter" pale mbele. Kaniki aliingizwa dakika 10 kabla mchezo kwisha unategemea nini? Saidi Maulidi alishindwa kabisa kufurukuta siku ile pia Shaabani Nditi.

Hata kabla ya mechi ya Jumamosi, wengi walitoa maoni yao kuwa timu yetu haina uwezo wa kufunga magoli. Kwa kifupi hatuna mfungaji/wafungaji wa kutegemea. Utasikia leo goli kafunga Badi Kassim, kesho Nizar Khalfan n.k. tena kagoli kamoja kati ya mechi tano au 10. Kweli kuna timu hapo? Kuna wafungaji hapo? NI KWELI TAIFA STARS UWEZO WAKE BADO MDOGO.

Saturday, April 14, 2007

SHULE ZIWE VITUVO VYA MAENDELEO

Mwaka huu sote tumeshuhudia ujenzi wa shule nyingi za SEKONDARI. Shule zimejengwa kwa AGIZO na kweli AGIZO limefanyiwa kazi. Na sasa Wilaya zinashindana na mikoa nayo inashindana kwa kujenga shule nyingi watoto wetu wengi wamepata nafasi ya kujiunga na shule za sekondari. Hilo ni jambo zuri. Ingawa baadhi yetu wanahoji kama kweli kujenga shule ndiyo kuwa na ubora wa Elimu? Sasa baada ya shule kujengwa tuzipatie vitendea kazi na tufuatilie kuona elimu bora inatolewa

Wazo langu la leo ni kwamba hizi shule za Sekondari zinazojengwa katika kila Kata ziwe chachu za maendeleo katika nchi yetu. Sekta zote zijikite katika Kata ziliko shule kwa ajili ya kutoa huduma na kujenga uchumi. Kwa kuwa naamini kuwa kwenye shule hizo kuna watu wa aina mbalimbali ambao wasingependa kuona kuwa wametupwa. Kwa mfano hakuna mwalimu yeyote ambaye angependa kufundisha na kuishi sehemu ambayo maji, usafiri, umeme, mawasiliano ni shida. Asingependa kuishi sehemu ambayo upatikanaji wa chakula ni shida, asingependa kuishi sehemu ambayo hakuna huduma ya afya.

Kama sekta zote zitajikita ziliko shule za sekondari ni rahisi kupanga mipango ya maendeleo yenye upeo mpana zaidi na itakuwa ni rahisi kufuatilia na kupima maendeleo. Watu watajifunza kutoka kwa wengine na maendeleo yataonekana. Haya ni maoni yangu.

Nakumbuka nilipokuwa mdogo sehemu zote zilizokuwa na "Middle Schools" huduma muhimu zilipatikana. Waalimu walionekana wamaana sana, waliheshimika na walikuwa na uwezo mzuri kimaisha. Ilikuwa ni sifa kuitwa mtoto wa mwalimu kwa sababu alikuwa ni kioo cha maisha mahali pale. Sasa je? TUFUFUE MTAZAMO HUO. TUZIFUATE SHULE ZA SEKONDARI KWA MAENDELEO.

"ZOGOWALE" WANAUME WANAFANYA KAZI MASAA 4

Hivi tumeshawahi kujipima katika jamii zetu katika utendaji kazi kati ya wanawake na wanaume?

Ili kuweza kufahamu ni akina nani hasa wanaotumia muda mwingi wa kufanya kazi?Hivi karibuni kikundi cha watafiti 10 kutoka Wizara ya Kilimo Chakula na Ushirika kilisafiri hadi kijiji/mtaa wa Zogowale, Wilaya ya Kibaha, Mkoa wa Pwani ili kuweza kujifunza masuala ya Jinsia katika kijiji hicho.

Watafiti hao walifanya majadiliano na wakazi wa mtaa huu wapatao 47. Baada ya kudodosana kwa takribani masaa mawili. Iligundulika kuwa, wanaume hutumia masaa manne kwa siku kwa kufanya kazi, wakati wanawake wao hutumia masaa 12! Eeh jamani tutafika kweli? Maendeleo yatapatikanaje kwa kufanya kazi kwa muda mchache namna hiyo na huku mwanamke akiachiwa shughuli nyingi za kufanya.Hata hivyo katika utafiti huo, ilibainika kuwa, jamii ya

Zogowale imeshaanza kubadilika, kwani kwa sasa zile ndoa changa zimeanza kusaidiana katika kufanya kazi. Wanaume huchota maji, hufua nguo na hata kupika chakula! Safi sana.Je, akina baba wanawapeleka watoto wao hospitali mara wanapougua ?(yaani kuwabeba kama wanavyofanya akina mama?). Akina baba wa Zogowale bado ni wazito kwa hilo. Wao hutoa amri tu na kutoa fedha za tiba, lakini si rahisi kumkuta baba kutoka Zogowale amebeba mtoto na kumpeleka hospitali!Kumenya mihogo je? Kazi hii nayo hufanywa na akina mama. Ni mara chache sana kukuta baba akimenya mihogo.

Zogowale, maisha huanza mapema, katika umri wa miaka 20 ni rahisi sana kumkuta kijana akiishi na mwanamke na pengine kuwa na mtoto hata mmoja!
Labels: John Banzi

Wanawake wapewe kipaumbele katika kutoa mikopo

Takribani miezi miwili sasa nimekuwa nikifuatilia kwa jinsi wanawake wa Tanzania wanavyojishughulisha katika kujipatia riziki.

Kwa mfano Jijini Dar Es Salaam baadhi ya akina mama ndiyo wanaolisha wafanyakazi wa jiji hili. Si mara moja ama mbili mimi mwenyewe nilipata msosi pale Tazara karibu na Redio Tanzania kwa akina mama hao. Wanawake wanaoendesha biashara ya mama lishe wengi wao ni vijana kati ya umri wa miaka 20-45 hivi.

Kuna hii biashara ya kuuza chupa za plastic jijini Dar. Akina mama wamo, shughuli hii hapa jijini hufanywa na wanawake wa umri mkubwa kati ya miaka 40-50. Pengine vijana wanaona aibu kupita mitaani kuokota chupa ndiyo maana hawaonekani sana kwenye biashara hiyo.Pengine huokota usiku! Lakini utazionaje chupa usiku? Wazee hawaoni haya wanachotaka ni riziki. Na ikumbukwe kuwa hawa wanabeba mzigo mkubwa katika kaya wengine huishi hata na wajukuu na watoto wa ndugu zao kwa hiyo la msingi wao ni kupata riziki. Aibu ya nini?

Pale Mbagala Rangi 3 ifikapo jioni kuanzia saa 12 biashara mbalimbali huanza kufanyika. Wapo wauza matunda na mbogamboga, wapo wauza mihogo, wapo wauza korosho n.k. Lakini wanaofanya biashara hizo wengi ni wanawake wa rika mbalimbali.

Nilipokuwa kwenye semina mjini Morogoro hivi karibuni niliwakuta wanawake wakiuza nguo za aina mbalimbali kando ya kumbi za mikutano. Na si mara moja kuwaona wanawake wakifanya biashara hizo kwenye kumbi mbalimbali za mikutano. Wapo Morogoro Hotel, wapo SUA, wapo Islamic University n.k.

Baada ya kufuatilia na kudadisi sana na kuangalia ile mikopo ya bilioni moja iliyotolewa kwa kila mkoa kwa ajili ya ujasiliamali. Napenda kushauri kuwa mikopo hiyo kipaumbele wapewe wanawake. Wanawake ni nguzo ya familia kwa kweli. Wanawake wakijikwamua kiuchumi maendeleo yatapatikana kwani waathirika wakubwa kiuchumi kwenye jamii zetu ni wanawake. Lakini jitahada zao kujikwamua kiuchumi zinaonekana. TUANZE SASA

Monday, March 12, 2007

USAFIRI DAR - JUMATATU

Leo nimeamua kuandika taabu ya usafiri wa daladala hapa DAR hasa siku ya Jumatatu.

Leo nimeamka saa 10.30 asubuhi ili niwahi usafiri wa kunifikisha Mbagala. Nilipata bus la kwenda Ubungo. Kabla ya kufika Mbagala Kizuiani tayari foleni ilishaanza. Na tulipofika Mbagala Mission gari moja dogo lilijichomeka kati ya bus letu na gari jingine kutoka mjini, ajali! Hapo ndipo shughuli ilipoaanza. Safari ikafa, tukarudishiwa fedha zetu. Mimi na abiria wengine tulianza kutembea kwa miguu.

Nilitembea hadi Mtoni kwa Aziz Ally kwani nilipofika Mtoni Mtongani kulikuwa na umati mkubwa wa watu ukisubiri usafiri. Nilipata usafiri wa kwenda Tandika. Nilipofika Tandika kwenye vituo vya mabus abiria walikuwa wamefurika usafiri bado ulikuwa shida. Nilipata usafiri wa kugombea na kupata kiti cha wanafunzi, kile kiti kinachounguza hadi niliposhuka pale Tazara-Kilimo. Nilikuwa nimeshachoka sana, nimelowa jasho sana na tayari ilishafika saa 1.45. Hiyo ndiyo adha ya usafiri DAR.

Monday, January 29, 2007

TUNATAKIWA KUFIKIRI KIDOGO TU

Tunatakiwa kufikiri kidogo tu ili kuweza kupunguza au kuondoa kabisa msongamano wa magari njia ya Kilwa. Nafahamu kuwa barabara ya Kilwa iko kwenye mpango wa kupanuliwa na kuifanya ya kisasa zaidi. Tuliahidiwa kuwa shughuli hiyo ingeenza mwezi Desemba 2006, lakini hadi hivi sasa, hali ni ile ile.

Huku tukisubiri kutengenezwa kwa mpango huu. Watumiaji wa barabara hiyo tufikiri kidogo tu. Hivi mashimo yaliyoko kwenye barabara hiyo yangezibwa vizuri tu hali ingekuwaje. Mashimo ya pale kwa Aziz Ally, Uwanja wa Sabasaba na pale Kurasini Mivinjeni yanakera sana na ni moja ya sababu ya msongamano barabara ya Kilwa. Kama kituo cha Mtoni Mtongani kingepanuliwa au kufanyiwa marekebisho msongamano usingekuwepo. Iwapo Halmashauri ya Temeke ingetengeneza ile barabara inayoanzia daraja la Tazara kwenda Tandika, kusingekuwa na sababu ya magari yanayoishia Tandika na hata yanayokwenda Buguruni, kupitia kwa Aziz Ally, msongamano ungepungua sana. Utaratibu mwingine ni kuyapangia magari ya mizigo muda tofauti. Ningependekeza yaanze shughuli zake kuanzia saa 3.00 asubuhi. Hivi sasa hakuna utaratibu maalum. Utakuta lori la mchanga, mkaa, magogo, tanker la mafuta, vipanya,"magobori" (DCM), Coaster, Suzuki, Pikipiki, baiskeli na waenda kwa miguu - barabara ni hiyo hiyo moja kweli patokosa msongamano hapo? Patakosa ajali hapo? Tunatakiwa tufikiri kidogo tu.

Monday, January 22, 2007

BENKI KUU SARAFU CHAKAVU NI KERO

Jana Jumapili nilisafiri kwenda Mikocheni kwa basi la daladala. Nilipkuwa narudi nyumbani kwangu nilipanda basi la Kawe-Mtoni Mtongani. Nauli ni Tshs 250/- nilipotoa fedha hizo kondakta aking'aka, mzee hiyo hizo shilingi 50 chukua mwenyewe imechakaa hata kusomeka haisomeki. Mimi nilikuwa sikuiangalia sawasawa. Niliporudishiwa nikagundua kuwa kweli ilikuwa imesuguliwa sehemu ya wale swala na picha ya Mwl.Nyerere lakini bado ilikuwa inasomeka shilingi 50. Nikamwambia sina hela nyingine kama hutaki shauri yako. Dereva akazima gari akatoka kwenye kiti chake kuja kugombana na mimi. Nilijaribu kuwaelimisha lakini waliikataa sarafu ile hadi nilipotoa fedha nyingine. Ndani ya basi kuna abiria walioniunga mkono na kuna walionibeza kuniona kama msumbufu!
Sarafu hizi zinazoonyesha kuchakaa kwa kweli ni nyingi na zinaleta usumbufu mkubwa hasa kwenye usafiri na hata unapotaka kununua vitu ambavyo si vya gharama kubwa. Mtu akishaiona tu anasema mimi sipokei hiyo sarafu.

Lakini tukumbuke kuwa sarafu hizo ziko kwenye mzunguko na siyo senti ni shilingi. Je kukiwa na sarafu za thamani ya shilingi 50 milioni 10 ni kiasi gani cha fedha ambacho watu wanasema si fedha wakati bado ziko kwenye mzunguko? Milioni 500 ni shule ngapi za msingi zingejengwa? BENKI KUU SARAFU CHAKAVU NI KERO ZIONDOENI KWENYE MZUNGUKO.

Tuesday, January 16, 2007

BILA UTAFITI TUNAJIDANGANYA

Aina ya gari mpya zinatoka, aina mpya za simu zinatengenezwa, kalamu mpya zinatengenezwa. Sisi kazi yetu kununua tu, kuagiza tu. Mimi nataka shangingi VX....., mimi naipenda kweli simu ya Nokia. Ndivyo tulivyo watanzania. Kazi yetu kununua tu, kununua tu. Tunaagiza tu. Wenzetu wanafikiri na kusonga mbele sisi tunaagiza tu.

Hivi kweli tumetoa kipaumbele kwenye utafiti wa sekta zote za uzalishaji? Mimi nakataa. Sindano tunaagiza, mashati tunaagiza, viatu tunaagiza hata kiwanja cha mpira tumeagiza (unakataa nini si wachina wametujengea, kwani tumebuni sisi?).

Wataalamu tunao lakini hatuwatumii. Hatuwatumii kwenye sekta za uzalishaji ili kuinua uchumi wetu hatuwatumii hata kushauri tu. Sisi tunapenda vitu rahisi rahisi. Wenzetu wafanye sisi tutumie. Kwa kifupi hatufanyi utafiti. Halafu si wavumilivu, tunakwepa sana gharama. Mtaalamu wa umwaguiliaji anaweza kushauri kuwa inawezekana kuweka miundo mbinu ya umwagiliaji na kuzalisha mpunga mara tatu kwa mwaka na kutoa magunia 50 kwa hekta lakini zinahitajika kiasi cha fedha Tshs 50 bilioni. Utasikia, mama, mama, mama fedha zote hizo zitatoka wapi we mtoto acha balaa lako. Badala ya kuuliza je utahitaji fedha hizo kutekeleza jambo hilo kwa kipindi gani? Hilo hatufikirii hata kidogo. Lakini tunaimba tutaondoa umasikini tutaondoa njaa. Hivi hivi tu. Kirahisi rahisi tu. Haiwezekani bwana. Maendeleo ni gharama.

Hatufanyi utafiti.Tunaogopa utafiti kwa sababu ni gharama. Wanasiasa hawapendi utafiti kwasababu hawaoni matunda ya haraka. Matokeo yake utafiti kwenye Kilimo umeduamaa, kwenye Afya ndiyo kabisa huko viwandani ni zero. Pengine kidogo wataalamu wa ujenzi wanajitahidi. Lakini kibinafsi. Mtu anabuni jengo na likijengwa basi tunakiri nakusema aa jengo hilo amelibuni Banzi! Lakini kama Taifa kwa ujumla wake tumesahau utafiti na Maendeleo.

Hakuna atakayetuondolea Malaria kama utafiti wa kina kuhusu Malaria hapa nchini hautafanyika. Hakuna atakayetuondolea njaa na umaskini kama tutapuuza utafiti katika kilimo. Nasema hakuna. Bila kufanya utafiti tunajidanganya kufikia maendeleo ya kweli.

PAMOJA NA KUONDOA WAMACHINGA-Dar bado chafu

Jumapili iliyopita nilitembelea Kariakoo, Ilala, Tandika, Mbagala na Temeke.
Tusidanganyane, Dar bado chafu. Kila nilipopita malundo ya taka yamejaa kibaa kando ya barabara kuu, uchochoroni, nyumba za watu na wakati mwingine hospitalini!

Pale kwenye maghorofa ya nyumba za "NHC" Ilala, maji taka yanatiririka hovyo, hovyo inabidi uwe mtaalamu wa kuruka viunzi ili usiyakanyage na kama umevaa ndala ndiyo hakuna pa kukwepa utakanyaga tu.

Haya, pale karibu kabisa na Hospitali ya Manispaa ya Temeke pale nje, karatasi kibao, nyingine ziko kwenye mifereji ya maji machafu.

Kule Tandika sokoni mambo ni yale yale, uchafu, uchafu, uchafu mpaka mtaa wa Bubu wote kuchafu!

Mtoni Mtongani karibu kabisa ya kituo cha mabasi ya daladala kuna lundo la uchafu na kibaya zaidi watu wanachakurachakura wakiokoteza vinavyowafaa na watu wanaangalia tu.

Nakutana na magari ya kuzoa uchafu, he, kichekesho. Mengine hayana taa za mbele yamechakaa choka mbaya lakini yanapita barabarani. Hivi kweli kuna sheria inayoruhusu magari ya kubeba uchafu yawe machakavu pia? Askari wa usalama barabarani wanaona hilo wanafumbia macho wao kazi yao kukamua magari ya mkaa na daladala. Ukikutana na magari hayo ziba pua. Hiyo harufu! Kibaya yanasomba uchafu na kudondosha uchafu barabarani.

Dar bado chafu, hata pale Kariakoo mitaa karibu yote ni michafu, nenda Tandamti, Sikukuu, Kongo, na Aggrey ni michafu.

Mimi najiuliza, tumewaondoa wamachinga sawa. Lakini mbona Jiji bado chafu? Hivi itachukua muda gani kuona "impact" ya kuwaondoa wamachinga hasa kwenye suala la usafi?

TUNANAKILI HATA MAJINA!

Enyi Watanzania wenzangu, leo nimeamua kuandika kuhusu tabia iliyozuka kwa baadhi yetu ya kutaka kunakili kila kitu (copying). Kibaya zaidi tunanakili hata majina!

Hebu fikiria mtu anaanzisha shule ya sekondari, pamoja na gharama zote alizogharamia, baadaye anaiita St. Mary's au St. Mathew. Hivi ndani ya vichwa vyetu kuna nini? Kuna ulazima wowote wa kuita Saint, Saint.

Na sisi wazazi tukiona shule inaitwa St.... basi vichwa juu. Mimi nitampeleka mtoto wangu St. Elizabeth, mwingine St. Anne, mwingine St.Luka. Hivi kuna siri gani na shule hizi zinazoanzia na St? Wizara inayohusika ilijibu hili. Pengine hizi hazilipi kodi au zinapoingiza vifaa vya shule huwa hazitozwi ushuru maana ni za watakatifu hizi!

Natumaini wengi wenu mtakubaliana nami kwamba miaka kumi iliyopita upuuzi kama huu haukuwepo. Wengine tumesoma Njombe Sekondari, Tosamaganga Sekondari, Ilboru Sekondari, Tambaza Sekondari, Kilakala Sekondari, Loleza Sekondari, Mkwawa Sekondari, Iyunga Sekondari . Hata Mh. Rais Jakaya Mrisho Kikwete amesoma Kibaha Sekondari. Shule zilikuwa nzuri tu, wanafunzi walikuwa wanafaulu vizuri tu. Tena ilikuwa fahari kusema mimi nasoma Tosamaganga Sekondari. Lakini siku hizi shule hizi zinazoitwa za binafsi na majina nayo yabinafsi kweli utasikia shule inaitwa California nyingine Mississippi mh hapa ndo tumefika. Au shule hizi zinapata misaada kutoka ng'ambo kama tulivyozoea? Misaada, misaada, misaada hata vyoo misaada kutoka Japan na wafadhili wanaweza kusema jina la choo kiitwe.......... maana ni msaada!

Shule umeijenga mwenyewe, kwanini usiite Shule ya Sekondari Jambuya?. Maana unajua maana yake, pengine Jambuya ni jina la babu yako utakuwa umemuenzi babu yako na kwakweli pengine dunia nzima kutakuwa na shule hiyo tu yenye jina hilo. "that is unique".

Ikiwa hata majina tunanakili tunachokiweza hasa ni kipi? Hebu wenzangu mnieleze. Wanaohusika hawajaliona hili au nao ndiyo wale washabiki wa St au California?

Tufikiri upya.

Tuesday, January 9, 2007

WATOTO WANAMATUMAINI YA MWAKA MPYA

Mwaka mpya huo.

Wengine mwaka mpya ndo mwanzo wa matatizo. Watoto wanataka kwenda shule, mfukoni kumekauka. Lakini kibaya zaidi kuna wengine waliozaliwa tarehe 1/1/ wanatakiwa kufanyiwa "birthday party". Usiniulize, mimi sikufanyiwa. Ila watoto wangu inabidi kuwafanyia.

Watoto wanamatumaini mapya. Kila mwaka mpya kwao ni mwanga mpya. Lakini wanatutegemea sana sisi wazazi wao kuwatayarishia njia. Watoto wetu wana matumaini ya kuishi maisha bora kuliko sisi. Hii inawezekana iwapo tutabadilika katika nyanja zote. Kikubwa turudishe maadili mema. Tuwalee watoto wetu kwa kufuata misingi ya dini na elimu dunia. Dini zote zinafundisha Upendo, Imani, Amani na Kusaidiana na Kusameheana.
Watoto hawa (pichani) kutoka kushoto Maggie Julius na Maria Mwaka Banzi wanafurahia mwaka mpya 2007.

HERI YA MWAKA MPYA

NIMERUDI KUTOKA MATOMBO!

HERI YA MWAKA MPYA!

Ndiyo, nimerudi kutoka Matombo. Matombo ya mwaka 2006, siyo ya 1970s.
Matombo ya sasa mambo kwa fedha tu. Huna sababu ya kubeba sukari kutoka Moro au Dar, huna sababu ya kununua khanga au kitenge kutoka Dar au Moro huna sababu ya kubeba bia wala soda. Mambo yote Matombo tu.

Matombo kumekucha, Matombo kumebadilika. Matombo mtandao wa Celtel unatamba huku nayo TTCL baba wa mawasiliano akionyesha kali yake.

Matombo sasa mambo kwa Solar kama si solar basi "generator" lakini siyo za Richmond! Watu wanaona TV, humdanganyi mtu. Ndiyo, hata World Cup mbona wenzio waliona "live." Unashangaa nini sasa?

Matombo bado ukarimu uko pale pale. Natoa zawadi ya thamani ya shilingi elfu mbili. Napata jogoo mkubwaa. Kila siku kuku tu. We acha tu. Kila siku ndizi, maembe, ubwabwa, mashelisheli, mafenesi, mananasi ni tafrija tupu!

Matombo imebadilika. Vijana wanaongelea kulima kitaalamu. Nakutana na Michael Mloka Tunywe, ananitembeza kwenye bustani yake aliyopanda migomba, minazi, minanasi, midimu natembea hadi nachoka baadaye ananiomba ushauri afanye nini?Lakini soko hakuna nanasi hadi shilingi mia moja unapata. Namshauri. Kweli inatia moyo.

Mfizigo nayo je bado ipo? Ah bado. Kijiji kimepiga marufuku uchimbaji wa madini kiholela bila kuzingatia hifadhi ya mazingira. Big up wazee wangu. Nilienda kupiga "solono" nikateleza, vidonda nimerudi navyo na kuvitibu pale St. Vincent Dispensary, Vikindu kwa masista-wakaniambia pole sana.

Matombo kumekucha, vijana wanajenga nyumba bora kwa kutumia matofali ya kuchoma na kuezeka kwa mabati. Kijiji cha Lumala kinatia fora, sasa mambo yanaelekea Utunu, Mng'ombe hadi Nyangala! Kiswira, Nige, Gubi, Mhangazi bati pweya!

Kanisani je. Kwaya ya Mtamba inaendelea kutia fora. Ndiyo waliopangiwa kuimba usiku wa Christmass. Walikuja kwa mbwembwe kwa kukodi Costa wakiimba kwa mbwembwe huku wakipambwa na T-SHIRT zenye nembo ya kanisa la Mt.Paul Matombo. Kanisa nililobatizwa, kupata Komunio hata Kipaimara. Hapa ndipo nilipotumikia kanisani katika ibada za misa takatifu.

Kiswira, hapa ndipo kwetu hapa ndipo nilipopata elimu yangu ya msingi. Makao Makuu ya klabu ya Mpira ya Kiswira. Klabu ambayo tuliijenga sisi wenyewe kwa kubeba matofali moja moja hata kama ni mdogo kiasi gani na kusaidiwa na Brother Rudolph aliyekuwa kiongozi wa kiwanda cha Mayungi kilichozalisha mafundi seremala wengi kutoka Matombo. Nguvu ya Kiwanda hicho ni kutoka kwenye maporomoko ya Mayungi. Nasikia maporomoko hayo yanaweza kuzalisha umeme wakutosha na kulisha tarafa nzima ya Matombo!

Watu wanakalia taarifa, tunategemea Richmond hadi Matombo ?Hatutofika!