Monday, January 29, 2007

TUNATAKIWA KUFIKIRI KIDOGO TU

Tunatakiwa kufikiri kidogo tu ili kuweza kupunguza au kuondoa kabisa msongamano wa magari njia ya Kilwa. Nafahamu kuwa barabara ya Kilwa iko kwenye mpango wa kupanuliwa na kuifanya ya kisasa zaidi. Tuliahidiwa kuwa shughuli hiyo ingeenza mwezi Desemba 2006, lakini hadi hivi sasa, hali ni ile ile.

Huku tukisubiri kutengenezwa kwa mpango huu. Watumiaji wa barabara hiyo tufikiri kidogo tu. Hivi mashimo yaliyoko kwenye barabara hiyo yangezibwa vizuri tu hali ingekuwaje. Mashimo ya pale kwa Aziz Ally, Uwanja wa Sabasaba na pale Kurasini Mivinjeni yanakera sana na ni moja ya sababu ya msongamano barabara ya Kilwa. Kama kituo cha Mtoni Mtongani kingepanuliwa au kufanyiwa marekebisho msongamano usingekuwepo. Iwapo Halmashauri ya Temeke ingetengeneza ile barabara inayoanzia daraja la Tazara kwenda Tandika, kusingekuwa na sababu ya magari yanayoishia Tandika na hata yanayokwenda Buguruni, kupitia kwa Aziz Ally, msongamano ungepungua sana. Utaratibu mwingine ni kuyapangia magari ya mizigo muda tofauti. Ningependekeza yaanze shughuli zake kuanzia saa 3.00 asubuhi. Hivi sasa hakuna utaratibu maalum. Utakuta lori la mchanga, mkaa, magogo, tanker la mafuta, vipanya,"magobori" (DCM), Coaster, Suzuki, Pikipiki, baiskeli na waenda kwa miguu - barabara ni hiyo hiyo moja kweli patokosa msongamano hapo? Patakosa ajali hapo? Tunatakiwa tufikiri kidogo tu.

Monday, January 22, 2007

BENKI KUU SARAFU CHAKAVU NI KERO

Jana Jumapili nilisafiri kwenda Mikocheni kwa basi la daladala. Nilipkuwa narudi nyumbani kwangu nilipanda basi la Kawe-Mtoni Mtongani. Nauli ni Tshs 250/- nilipotoa fedha hizo kondakta aking'aka, mzee hiyo hizo shilingi 50 chukua mwenyewe imechakaa hata kusomeka haisomeki. Mimi nilikuwa sikuiangalia sawasawa. Niliporudishiwa nikagundua kuwa kweli ilikuwa imesuguliwa sehemu ya wale swala na picha ya Mwl.Nyerere lakini bado ilikuwa inasomeka shilingi 50. Nikamwambia sina hela nyingine kama hutaki shauri yako. Dereva akazima gari akatoka kwenye kiti chake kuja kugombana na mimi. Nilijaribu kuwaelimisha lakini waliikataa sarafu ile hadi nilipotoa fedha nyingine. Ndani ya basi kuna abiria walioniunga mkono na kuna walionibeza kuniona kama msumbufu!
Sarafu hizi zinazoonyesha kuchakaa kwa kweli ni nyingi na zinaleta usumbufu mkubwa hasa kwenye usafiri na hata unapotaka kununua vitu ambavyo si vya gharama kubwa. Mtu akishaiona tu anasema mimi sipokei hiyo sarafu.

Lakini tukumbuke kuwa sarafu hizo ziko kwenye mzunguko na siyo senti ni shilingi. Je kukiwa na sarafu za thamani ya shilingi 50 milioni 10 ni kiasi gani cha fedha ambacho watu wanasema si fedha wakati bado ziko kwenye mzunguko? Milioni 500 ni shule ngapi za msingi zingejengwa? BENKI KUU SARAFU CHAKAVU NI KERO ZIONDOENI KWENYE MZUNGUKO.

Tuesday, January 16, 2007

BILA UTAFITI TUNAJIDANGANYA

Aina ya gari mpya zinatoka, aina mpya za simu zinatengenezwa, kalamu mpya zinatengenezwa. Sisi kazi yetu kununua tu, kuagiza tu. Mimi nataka shangingi VX....., mimi naipenda kweli simu ya Nokia. Ndivyo tulivyo watanzania. Kazi yetu kununua tu, kununua tu. Tunaagiza tu. Wenzetu wanafikiri na kusonga mbele sisi tunaagiza tu.

Hivi kweli tumetoa kipaumbele kwenye utafiti wa sekta zote za uzalishaji? Mimi nakataa. Sindano tunaagiza, mashati tunaagiza, viatu tunaagiza hata kiwanja cha mpira tumeagiza (unakataa nini si wachina wametujengea, kwani tumebuni sisi?).

Wataalamu tunao lakini hatuwatumii. Hatuwatumii kwenye sekta za uzalishaji ili kuinua uchumi wetu hatuwatumii hata kushauri tu. Sisi tunapenda vitu rahisi rahisi. Wenzetu wafanye sisi tutumie. Kwa kifupi hatufanyi utafiti. Halafu si wavumilivu, tunakwepa sana gharama. Mtaalamu wa umwaguiliaji anaweza kushauri kuwa inawezekana kuweka miundo mbinu ya umwagiliaji na kuzalisha mpunga mara tatu kwa mwaka na kutoa magunia 50 kwa hekta lakini zinahitajika kiasi cha fedha Tshs 50 bilioni. Utasikia, mama, mama, mama fedha zote hizo zitatoka wapi we mtoto acha balaa lako. Badala ya kuuliza je utahitaji fedha hizo kutekeleza jambo hilo kwa kipindi gani? Hilo hatufikirii hata kidogo. Lakini tunaimba tutaondoa umasikini tutaondoa njaa. Hivi hivi tu. Kirahisi rahisi tu. Haiwezekani bwana. Maendeleo ni gharama.

Hatufanyi utafiti.Tunaogopa utafiti kwa sababu ni gharama. Wanasiasa hawapendi utafiti kwasababu hawaoni matunda ya haraka. Matokeo yake utafiti kwenye Kilimo umeduamaa, kwenye Afya ndiyo kabisa huko viwandani ni zero. Pengine kidogo wataalamu wa ujenzi wanajitahidi. Lakini kibinafsi. Mtu anabuni jengo na likijengwa basi tunakiri nakusema aa jengo hilo amelibuni Banzi! Lakini kama Taifa kwa ujumla wake tumesahau utafiti na Maendeleo.

Hakuna atakayetuondolea Malaria kama utafiti wa kina kuhusu Malaria hapa nchini hautafanyika. Hakuna atakayetuondolea njaa na umaskini kama tutapuuza utafiti katika kilimo. Nasema hakuna. Bila kufanya utafiti tunajidanganya kufikia maendeleo ya kweli.

PAMOJA NA KUONDOA WAMACHINGA-Dar bado chafu

Jumapili iliyopita nilitembelea Kariakoo, Ilala, Tandika, Mbagala na Temeke.
Tusidanganyane, Dar bado chafu. Kila nilipopita malundo ya taka yamejaa kibaa kando ya barabara kuu, uchochoroni, nyumba za watu na wakati mwingine hospitalini!

Pale kwenye maghorofa ya nyumba za "NHC" Ilala, maji taka yanatiririka hovyo, hovyo inabidi uwe mtaalamu wa kuruka viunzi ili usiyakanyage na kama umevaa ndala ndiyo hakuna pa kukwepa utakanyaga tu.

Haya, pale karibu kabisa na Hospitali ya Manispaa ya Temeke pale nje, karatasi kibao, nyingine ziko kwenye mifereji ya maji machafu.

Kule Tandika sokoni mambo ni yale yale, uchafu, uchafu, uchafu mpaka mtaa wa Bubu wote kuchafu!

Mtoni Mtongani karibu kabisa ya kituo cha mabasi ya daladala kuna lundo la uchafu na kibaya zaidi watu wanachakurachakura wakiokoteza vinavyowafaa na watu wanaangalia tu.

Nakutana na magari ya kuzoa uchafu, he, kichekesho. Mengine hayana taa za mbele yamechakaa choka mbaya lakini yanapita barabarani. Hivi kweli kuna sheria inayoruhusu magari ya kubeba uchafu yawe machakavu pia? Askari wa usalama barabarani wanaona hilo wanafumbia macho wao kazi yao kukamua magari ya mkaa na daladala. Ukikutana na magari hayo ziba pua. Hiyo harufu! Kibaya yanasomba uchafu na kudondosha uchafu barabarani.

Dar bado chafu, hata pale Kariakoo mitaa karibu yote ni michafu, nenda Tandamti, Sikukuu, Kongo, na Aggrey ni michafu.

Mimi najiuliza, tumewaondoa wamachinga sawa. Lakini mbona Jiji bado chafu? Hivi itachukua muda gani kuona "impact" ya kuwaondoa wamachinga hasa kwenye suala la usafi?

TUNANAKILI HATA MAJINA!

Enyi Watanzania wenzangu, leo nimeamua kuandika kuhusu tabia iliyozuka kwa baadhi yetu ya kutaka kunakili kila kitu (copying). Kibaya zaidi tunanakili hata majina!

Hebu fikiria mtu anaanzisha shule ya sekondari, pamoja na gharama zote alizogharamia, baadaye anaiita St. Mary's au St. Mathew. Hivi ndani ya vichwa vyetu kuna nini? Kuna ulazima wowote wa kuita Saint, Saint.

Na sisi wazazi tukiona shule inaitwa St.... basi vichwa juu. Mimi nitampeleka mtoto wangu St. Elizabeth, mwingine St. Anne, mwingine St.Luka. Hivi kuna siri gani na shule hizi zinazoanzia na St? Wizara inayohusika ilijibu hili. Pengine hizi hazilipi kodi au zinapoingiza vifaa vya shule huwa hazitozwi ushuru maana ni za watakatifu hizi!

Natumaini wengi wenu mtakubaliana nami kwamba miaka kumi iliyopita upuuzi kama huu haukuwepo. Wengine tumesoma Njombe Sekondari, Tosamaganga Sekondari, Ilboru Sekondari, Tambaza Sekondari, Kilakala Sekondari, Loleza Sekondari, Mkwawa Sekondari, Iyunga Sekondari . Hata Mh. Rais Jakaya Mrisho Kikwete amesoma Kibaha Sekondari. Shule zilikuwa nzuri tu, wanafunzi walikuwa wanafaulu vizuri tu. Tena ilikuwa fahari kusema mimi nasoma Tosamaganga Sekondari. Lakini siku hizi shule hizi zinazoitwa za binafsi na majina nayo yabinafsi kweli utasikia shule inaitwa California nyingine Mississippi mh hapa ndo tumefika. Au shule hizi zinapata misaada kutoka ng'ambo kama tulivyozoea? Misaada, misaada, misaada hata vyoo misaada kutoka Japan na wafadhili wanaweza kusema jina la choo kiitwe.......... maana ni msaada!

Shule umeijenga mwenyewe, kwanini usiite Shule ya Sekondari Jambuya?. Maana unajua maana yake, pengine Jambuya ni jina la babu yako utakuwa umemuenzi babu yako na kwakweli pengine dunia nzima kutakuwa na shule hiyo tu yenye jina hilo. "that is unique".

Ikiwa hata majina tunanakili tunachokiweza hasa ni kipi? Hebu wenzangu mnieleze. Wanaohusika hawajaliona hili au nao ndiyo wale washabiki wa St au California?

Tufikiri upya.

Tuesday, January 9, 2007

WATOTO WANAMATUMAINI YA MWAKA MPYA

Mwaka mpya huo.

Wengine mwaka mpya ndo mwanzo wa matatizo. Watoto wanataka kwenda shule, mfukoni kumekauka. Lakini kibaya zaidi kuna wengine waliozaliwa tarehe 1/1/ wanatakiwa kufanyiwa "birthday party". Usiniulize, mimi sikufanyiwa. Ila watoto wangu inabidi kuwafanyia.

Watoto wanamatumaini mapya. Kila mwaka mpya kwao ni mwanga mpya. Lakini wanatutegemea sana sisi wazazi wao kuwatayarishia njia. Watoto wetu wana matumaini ya kuishi maisha bora kuliko sisi. Hii inawezekana iwapo tutabadilika katika nyanja zote. Kikubwa turudishe maadili mema. Tuwalee watoto wetu kwa kufuata misingi ya dini na elimu dunia. Dini zote zinafundisha Upendo, Imani, Amani na Kusaidiana na Kusameheana.
Watoto hawa (pichani) kutoka kushoto Maggie Julius na Maria Mwaka Banzi wanafurahia mwaka mpya 2007.

HERI YA MWAKA MPYA

NIMERUDI KUTOKA MATOMBO!

HERI YA MWAKA MPYA!

Ndiyo, nimerudi kutoka Matombo. Matombo ya mwaka 2006, siyo ya 1970s.
Matombo ya sasa mambo kwa fedha tu. Huna sababu ya kubeba sukari kutoka Moro au Dar, huna sababu ya kununua khanga au kitenge kutoka Dar au Moro huna sababu ya kubeba bia wala soda. Mambo yote Matombo tu.

Matombo kumekucha, Matombo kumebadilika. Matombo mtandao wa Celtel unatamba huku nayo TTCL baba wa mawasiliano akionyesha kali yake.

Matombo sasa mambo kwa Solar kama si solar basi "generator" lakini siyo za Richmond! Watu wanaona TV, humdanganyi mtu. Ndiyo, hata World Cup mbona wenzio waliona "live." Unashangaa nini sasa?

Matombo bado ukarimu uko pale pale. Natoa zawadi ya thamani ya shilingi elfu mbili. Napata jogoo mkubwaa. Kila siku kuku tu. We acha tu. Kila siku ndizi, maembe, ubwabwa, mashelisheli, mafenesi, mananasi ni tafrija tupu!

Matombo imebadilika. Vijana wanaongelea kulima kitaalamu. Nakutana na Michael Mloka Tunywe, ananitembeza kwenye bustani yake aliyopanda migomba, minazi, minanasi, midimu natembea hadi nachoka baadaye ananiomba ushauri afanye nini?Lakini soko hakuna nanasi hadi shilingi mia moja unapata. Namshauri. Kweli inatia moyo.

Mfizigo nayo je bado ipo? Ah bado. Kijiji kimepiga marufuku uchimbaji wa madini kiholela bila kuzingatia hifadhi ya mazingira. Big up wazee wangu. Nilienda kupiga "solono" nikateleza, vidonda nimerudi navyo na kuvitibu pale St. Vincent Dispensary, Vikindu kwa masista-wakaniambia pole sana.

Matombo kumekucha, vijana wanajenga nyumba bora kwa kutumia matofali ya kuchoma na kuezeka kwa mabati. Kijiji cha Lumala kinatia fora, sasa mambo yanaelekea Utunu, Mng'ombe hadi Nyangala! Kiswira, Nige, Gubi, Mhangazi bati pweya!

Kanisani je. Kwaya ya Mtamba inaendelea kutia fora. Ndiyo waliopangiwa kuimba usiku wa Christmass. Walikuja kwa mbwembwe kwa kukodi Costa wakiimba kwa mbwembwe huku wakipambwa na T-SHIRT zenye nembo ya kanisa la Mt.Paul Matombo. Kanisa nililobatizwa, kupata Komunio hata Kipaimara. Hapa ndipo nilipotumikia kanisani katika ibada za misa takatifu.

Kiswira, hapa ndipo kwetu hapa ndipo nilipopata elimu yangu ya msingi. Makao Makuu ya klabu ya Mpira ya Kiswira. Klabu ambayo tuliijenga sisi wenyewe kwa kubeba matofali moja moja hata kama ni mdogo kiasi gani na kusaidiwa na Brother Rudolph aliyekuwa kiongozi wa kiwanda cha Mayungi kilichozalisha mafundi seremala wengi kutoka Matombo. Nguvu ya Kiwanda hicho ni kutoka kwenye maporomoko ya Mayungi. Nasikia maporomoko hayo yanaweza kuzalisha umeme wakutosha na kulisha tarafa nzima ya Matombo!

Watu wanakalia taarifa, tunategemea Richmond hadi Matombo ?Hatutofika!

Thursday, December 21, 2006

NI KWELI HALMASHAURI ZA WILAYA ZINAPOTEZA MAPATO

LEO asubuhi nikiwa kwenye bus litokalo Mkuranga kwenda Mbagala, tulipofika Vikindu (Kwenye kizuizi cha kukagua mazao, madini, na raslimali nyingine). Kuna abiria aliyekuwa na mzigo wa kulipia ushuru sifahamu ni mzigo gani. Basi watoza ushuru hao wa Vikindu walimwambia alipe Tshs 900/= abiria huyo alitoa chapchap wala bila kudai stakabadhi ya malipo na gari hilo likaondoka!

Kwa hakika nilimuona mtoza ushuru yule akiweka noti ya Tshs 500/= kwenye shati lake. Nikajiuliza ni kiasi gani cha mapato kinapotea kwa njia hii? Ni mamilioni. Hatuwezi kuendelea kwa njia hii. Ni hatari, hakuna usimamizi mzuri pale. Na hii ni kwa Vikindu tu. Je kuna vituo vingapi vya aina hii vinavyopoteza mapato kirahisi rahisi tu nchi nzima?

Lakini tatizo liko kwa walipaji, wao wanafikiri aa shs 900 tu mbona kidogo! Je, kwa mwezi wakitokea watu 20,000 ambao hawakupewa stakabadhi ya malipo. Halmshauri ya Mkuranga kwa kizuizi cha Vikindu kitakuwa limepoteza milioni 18! Si haba. Ni madarasa mangapi hayo ya shule ya msingi yangejengwa kwa mwezi, kwa fedha za Vikindu tu? Tuwe makini.

Tuna uwezo wa kuendelea, tatizo ni sisi wenyewe.

Chrsitmass njema.

Nitakuwa Matombo, Morogoro kwa muda wa majuma mawili. Naenda kula "mwidu" na "komola."

Wednesday, December 20, 2006

SOKONI KARIAKOO NI TOPE TUPU

Leo mchana nimetokea maeneo ya Kariakoo. Nilipita kabisa karibu na Soko la Kariakoo. Huwezi kuamini, soko hilo tunalojivunia kuwa ni la Kimataifa, hakuna kitu ni tope tupu. Mvua inayoendelea kunyesha hapa Dar es Salaam kwa kweli ni hatari tupu kwa afya zetu. Hebu fikiria mwenyewe karibu mboga na matunda hushushwa sokoni kariakoo na kwenyewe ni kuchafu sasa kweli tutapona?

Miundo mbinu inayolizunguka soko hilo pia ni mibovu, barabara zimechimbika, mitaro imeziba. Lakini waswahili wako pembeni wanajichana chips tu! Umeme nao hakuna, majenereta yanaunguruma, nyumba zinaendelea kujengwa, mikokoteni nayo inakusukuma. Daladala zilizochanika viti basi shida tu. Hili ndilo jiji la DAR ES SALAAM.

Jiji? Rekebisheni mambo hapo kariakoo, ni aibu.

KWAHERI NATHANIEL KATINILA

Msiba mkubwa umetupata Wizara ya Kilimo Chakula na Ushirika, Ofisi ya Waziri Mkuu na Programu ya Kuendeleza Masoko ya Kilimo (AMSDP) kwa kuondokewa na mmoja kati ya vijana waliobobea katika fani ya kilimo naye si mwingine bali ni Marehemu Nathaniel Katinila (45) juma lililopita. Marehemu alifariki kwa ajali ya Ndege Cessna 5HTZ mali ya Tanzair iliyotokea Mbeya tarehe 16/12/2006.

Mimi namfahamu sana Katinila. Mwaka 1981 tulikutana pale MATI- Ukiriguru mimi nikiwa mwaka wa pili (DIP - CROP PRODUCTION) naye akiwa amekuja kuanza kozi hiyo hiyo. Baada ya kuhitimu masomo yake akafanya kazi miaka michache (sifahamu ni sehemu gani) baadaye akajiunga na Chuo Kikuu cha Sokoine ambako alipata shahada yake ya kwanza yenye mchepuo wa Uchumi Kilimo. Tulikutana tena mwaka 1993 katika Wizara ya Kilimo na Mifugo, Idara ya Utafiti na Mafunzo, yeye akiwa ARI-Naliendele Mtwara nami nikiwa Makao Makuu Dar Es Salaam wote tukiwa wachumi kilimo mwenzangu "Kati" (Nilizoea kumwita hivyo) akiwa kwenye programu ya "Farming Systems Research and Socio-Economics" nami nikiwa kwenye Kitengo cha Mipango, Kupelemba na Kutathmini (Planning, Monitoring and Evaluation).

Tukiwa pale Ukiriguru, wote tulishiriki kwenye kikundi cha maigizo kilichojulikana kama "MAJOSA" chini ya mwalimu wetu Benito Mwenda ambaye alikuwa mwanachuo mwenzetu ingawa kwa sasa ni Mkufunzi hapo hapo MATIU. Tukiwa chuoni Katinila alikuwa pia "Boxer."

Akiwa Naliendele amefanya kazi nyingi za utafiti katika masuala ya farming systems. Baadaye alijiunga na mradi wa " RIPS" uliokuwa ukiendeshwa mikoa ya kusini kabla ya kurudi tena Kilimo pale Naliendele.

Mara tu ilipoanzishwa Programu ya Kuendeleza Masoko ya Kilimo. Nathaniel alibahatika kuwa Mratibu wake wa Kwanza.

Namfahamu sana Katinila kwa mema yake kuliko mabaya. Alikuwa mshauri mzuri, mpole na asiye na pupa. MUNGU AIWEKE MAHALI PEMA PEPONI ROHO YA NATHANIEL KATINILA. AMINA.

Thursday, December 14, 2006

"UCHAWI WA SYRIA"

Mhandisi Phillip Mbuligwe amerudi leo leo kutoka Syria. Eeeh Mbuligwe, habari za Waarabu? Namuuliza tena kwa utani. "Acha wee Banzi, wale si Waarabu, wamepiga hatua kubwa kimaendeleo, siyo kama unavyofikiria wewe. Mimi nafikiri umezoea waarabu wa hapa "Bongo".

Ndiyo, Mbuligwe ni mhandisi. Mwezi Novemba, 2006 alikuwa kule Syria kwa mafunzo ya muda mfupi kuhusu umwagiliaji. Kwa maelezo yake, Phillip anasema kuwa, Syria hupata mvua mm 100 kwa mwaka, lakini wanajitosheleza kwa chakula. "Uchawi" mkubwa unaotumika kule ni umwagiliaji ndugu yangu anasema Phillip.

Umwagiliaji ni asilimia 100% katika kilimo. Siamini, naendelea kumdadisi. Sasa, mbona nasikia kule ardhi ni mchanga mtupu? Ni kweli, anaendelea kueleza Mbuligwe, Wasyria hufanya kila linalowezekana kupata maji. Huchimba visima virefu na pia hutumia maji ya mito inayokatiza katika ardhi yao. Serikali ilichofanya ni kutengeneza miundo mbinu ya umwagiliaji na kuendesha utafiti wa hali ya juu katika umwagiliaji.

Syria hutumia sana "Drip Irrigation" na "Sprinklers." Kwa njia hii wanatumia maji kufuatana na mahitaji ya mmea na maji hayapotei bure na kwakweli wakulima wanasema inalipa. Bila umwagiliaji, Syria isingeweza kuendesha kilimo.

Ndiyo, sasa wanalima mazao gani? Naendelea kumhoji. Aah Banzi kule kunastawi mazao mengi tu. Mbogamboga, ngano, matunda na hata mahindi. Lakini zao la chakula Syria ni ngano. Banzi, tikitimaji la Syria ni tamu utafikiri limewekwa asali anamalizia Mbuligwe.

Ndiyo, mtaalamu ndiyo huyo, amerudi toka Syria, amenieleza kuwa amejifunza mengi tena si kwa kuona tu au masomo ya nadharia, mafunzo yaliendeshwa kwa vitendo pia. Mbuligwe amerudi tumtumie kwenye utaalamu wa umwagiliaji.

Nilishawahi kusoma moja ya makala za Padri Privatus Karugendo (Kwa kweli huwa nasoma sana makala zake) anayeandikia gazeti la Rai. Katika makala hiyo, Karugendo anahoji, hivi kweli tumeshindwa kutumia vyanjo vyetu vya maji kwa umwagiliaji? Nafikiri vipaumbele vyetu vina walakini. Tujifunze basi kutoka Syria- 100 mm za mvua kwa mwaka, wanajitosheleza kwa chakula na "Tikitimaji ni tamu sana."

Wednesday, December 13, 2006

BANGO LA PAROKIA YA MAKUBURI CHA MDORI!

Jumapili iliyopita nilitembelea eneo la "External" kule Mabibo sehemu inayojulikana kwa jina la Makuburi hapa jijini Dar Es Salaam. Kwa bahati nilipita karibu kabisa na Kanisa Katoliki la Makuburi(Enuerete Mwenye Heri- Mtanisahihisha wasomaji).

Kilichonishangaza, kwanza si rahisi kufahamu kuwa hilo ndilo Kanisa Katoliki la Makuburi kama nilivyoandika hapo juu. Kuna maandishi madogo sana ambayo ukipita kwa mbali hayawezi kusomeka halafu yameandikwa hovyo hovyo tu. Hayapendezi! Lakini karibu na maandishi hayo kuna maandishi makubwa kwenye ukuta yanayosomeka kuwa Computer Training Centre. Sasa nikajiuliza hapa shughuli kubwa ni training au kuabudu?

Waumini wa Makuburi, Katekesta, Paroko nawaulizeni hivi kweli mmeshindwa kuandika bango linaloonyesha Parokia yenu? Nafahamu Makuburi ni moja ya Parokia ambazo mnatoa sadaka kwa wingi siku za dominika, mavuno na michango mingine. Hivi Bango kwenu si muhimu? Aaa jamani andikeni bango jingine zuri lenye herufi za kusomeka. Tena msimike sehemu zile muhimu kama vile kwenye vituo vya "External" na "Garage" barabara ya Mandela na pale kanisani penyewe. Nafikiri mtafanya hivyo kabla ya Christmass. Nitapita tena, na kama bado nitaandika mbado!

EL SAEDY BUS MNABOA KINOMA!

Kwa wale waliopata bahati ya kusafiri kwenda Kilosa mkoani Morogoro si rahisi kulikwepa bus la EL-SAEDY.

Mwezi uliopita nilisafiri kwenda Ilonga Kilosa kuhudhuria harusi ya rafiki yangu Alphonce Kadeng'uka (Hongera sana KADE!). Baada ya kuanganisha mabus mawili hadi kufika Ilonga, bus la mwisho nilililopanda lilikuwa ni la El- SAEDY kubwa.

Nasema mnaboa kinoma, kwanza kondakta alinipa ticket ambayo haikuonyesha mmiliki wa Bus na namba ya gari. Lakini nilimezea tu mradi kufika.Hata nauli natumaini walinilangua, sawa tu. Lakini nilipoangalia karibu namlango nikakuta maandishi "SitAfu Kiti"(Ikiwa na maana ya Staff Seat) halafu amechanganya herufi kubwa na ndogo. Lakini mmiliki anaona ni sawa na abiria nao hivyo hivyo, traffic hivyo hivyo! Kweli mnaboa. Si ingeandikwa tu kwa kiswahili kuwa ni kiti cha mfanyakazi. Hata namba za viti zimeandikwa hovyo hovyo (kichefu chefu). Kumbukeni gari hilo limenunuliwa kwa mamilioni ya shilingi kwanini mnalichezea chezea hovyo. Rekebisheni haraka. Noma wazee

TICKETS ZA DALADALA TUNALIWA

Nafikiri wengi wetu tuishio hapa Dar usafiri wetu unategemea zaidi magari ya abiria yajulikanayo kama Daladala. Unaposafiri kwenye gari hilo unatakiwa upewe ticket inayoonyesha kiasi cha nauli kwa safari yako namba ya gari, mmiliki wa gari na tarehe ya kusafiri.

Wamiliki wa magari hayo wengi hutoa ticket hizo lakini cha kushangaza ticket hizo ni vipande vya karatasi vilivyokwishatumika kwa shughuli nyingine. Utakuta umepata ticket lakini nyuma inaonyesha mshahara wa mtu au mambo mengine kabisa ambayo hayana uhusiano na usafiri.

Hivi kweli wanaomiliki magari hayo wanafahamu maana ya ticket? Je, SUMTRA wanakagua ticket hizo? Ushauri wangu ni kwamba ticket zote za Daladala ziwe na "format" moja na kuwe na rangi tofauti kwa njia tofauti. Ikiwezekana ziwe na alama ya kuingia au kutoka kwenye kituo kilichopangiwa. Huu ndiyo ustaarabu au mpangilio mzuri. Ninakerwa sana nipolipa nauli yangu nakupewa karatasi isiyo namaana lakini naambiwa eti ni ticket!

Tuesday, December 12, 2006

HIVI NI KWELI MIAKA 45 YA UHURU SEKTA YA KILIMO HAIJAFANYA LOLOTE?

Siamini kuwa miaka 45 tangu tupate UHURU wetu hakuna mafanikio kwenye sekta ya kilimo. Mafanikio yametajwa tu kwenye Elimu, Ujenzi wa Barabara kwa sababu ni rahisi kupima! Tusiwe wavivu jamani. Kweli hakuna viashiria kwenye sekta ya kilimo vinavyoonyesha mafanikio?

Imekuwa ni desturi sasa kuwa kila inapotayarishwa taarifa ya nchi hasa inapohusu mambo chanya, sekta ya Kilimo (mazao na mifugo) haimo. Ikumbukwe kuwa sekta hii inaajiri asilimia 80 ya watanzania na kulisha asilimia 100 ya watanzania sasa inawezekana vipi kutokuwa na mafanikio.

Kuna tatizo. Tatizo lipo kwa wale wanaokusanya taarifa na kuzitayarisha. Huenda hawajishughulishi kuweza kufahamu Kilimo imefanya nini. Mimi nina uhakika kuwa Kilimo imefanya mambo mengi kwenye masuala ya utafiti, umwagiliaji na mafunzo ukilinganisha kabla ya kupata uhuru. Hata uzalishaji umeongezeka pia kwa baadhi ya mazao na kuna mazao ambayo sasa yana umuhimu mkubwa katika taifa kuliko ilivyokuwa hapo awali(Kabla ya UHURU) uzalishaji wa maua ambao umeliingizia taifa fedha nyingi za kigeni. Lakini waliomwandikia Rais wetu mafanikio ya nchi miaka 45 baada ya UHURU wamepuuza hayo. Nchi imewekeza fedha nyingi sana kwenye sekta hiyo haiwezekanai kutokuwa na mafanikio. Unapozungumzia vyuo vikuu. Kwanini usiseme kuwa kuna Chuo Kikuu cha Sokoine ambacho kinatoa taaluma za sayansi ya kilimo ambapo kabla ya UHURU hatukuwa nacho. Huko unaweza kupata wataalamu wa Kilimo waliozalishwa na chuo hicho ambao wanafanya kazi ndani na nje ya nchi. Je, hayo siyo mafanikio ya nchi katika sekta ya Kilimo? Kuna mengi. Tusiwe wavivu katika kutayarisha taarifa.

MTOTO AMEZALIWA - nolema.blogspot.com

Mtoto amezaliwa leo tarehe 12/12/2006. Mtoto huyu anaitwa "BABA WA SHIRIKISHI"
Mzazi wa mtoto huyu ni Orgenness Lema. Karibu sana mtoto kwenye ulimwengu wa Blog. Kuna kaka yako "Banzi wa Moro" aliyekutangulia mwezi mmoja uliopita. Kuna kaka zako wakubwa kama vile, Ndesanjo Macha, Michuzi, Mjengwa, Jeff, Mongi na wengine wengi waone watakutunza.

Karibu sana

Thursday, December 7, 2006

HATUJAMFIKIA MKULIMA -WASSIRA

Waziri wa Kilimo Chakula na Ushirika Mh. Stephen Wassira amesema bayana kuwa wafanyakazi wa kilimo bado hawajamfikia mkulima. Mh.Wassira aliyasema hayo alipokutana kwa mara ya kwanza na wafanyakazi wa Wizara hiyo walioko Makao Makuu - Temeke Veterinary, tarehe 1/12/2006, Ijumaa.

Akiongea na wafanyakazi hao kwa muda usiozidi dakika 15. Waziri Wassira alisema kuwa, Wizara ina majukumu makuu mawili (1). Inatoa ajira kwa asilimia 80 ya Watanzania (2). Inawajibika kuhakikisha kuwa asilimia 100 ya watanzania wanapata chakula cha kutosha wakati wote.

Waziri alitoa changamoto kwa wafanyakazi hao kwa
- kumfikia mkulima kijijini ili aweze kupata mapato halisi kutokana na kilimo
- kufanya kila linalowezekana ili kuhakikisha kuwa watanzania wanapata chakula.

Aliwashauri wafanyakazi wote kuchapa kazi na kusema kuwa hakuna kazi isiyokuwa na maana na mshahara anaolipwa kwa kila mfanyakazi ni gharama kwa hiyo ni lazima kufanya kazi kwa pamoja ili Wizara iweze kutimiza malengo yake.

Kabla ya kuanza mazungumzo na wafanyakazi hao, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Mh. Peniel Lyimo alitoa taarifa kwa Waziri kuwa, Wizara ina jumla ya wafanyakazi 2,600. Kati ya hao wafanyakazi 1,165 wako kwenye Idara ya Utafiti na Mafunzo. Ni wafanyakazi 400 tu ndiyo wanaofanya kazi Makao Makuu ya Wizara.

Kikao hicho cha muda Mfupi kilihudhuriwa pia na Naibu Waziri wa Kilimo na Chakula Mh. Dr. David Matayo David na Naibu Katibu Mkuu Mh. Mohamed Muya.

Hii ni mara ya tatu kwa Waziri Wassira kuiongoza wizara hiyo. Mwaka 1973 aliteuliwa kuwa Naibu Waziri , Wizara ya Kilimo akiwa na umri wa miaka 27. Mwaka 1989 alirudi tena kwenye Wizara hiyo akiwa Waziri na mwaka huu mwezi Oktoba Rais Jakaya Mrisho Kikwete amempa jukumu la kuiongoza wizara hiyo.

KUPASISHA MBEGU MPYA (SEED RELEASE)

Ndiyo, kuna mdau mmoja amekuja na hoja kuwa kwanini wataalamu wa kilimo huwa wanasema kuwa wametoa mbegu mpya lakini wakulima wanalalamika kuwa mbegu hizo hazipatikani. Mdau huyu alikuwa na maana ya "seed release" akitafsiri kwa kiswahili kuwa ni kutoa mbegu. Ukweli ni kwamba hapa mbegu inapasishwa tayari kwa matumizi kisheria.

Mchakato wa uzalishaji mbegu za mazao kwa kweli unatumia muda mwingi, utaalamu mbalimbali na nyenzo mbalimbali ambazo waliobobea huchukua miaka mingi kufuzu utaalamu huo na wakisha fuzu wanajulikana kuwa wataalamu wazalishaji vipando (plant breeders). Kabla mbegu haijatolewa kutumika, hufanyiwa tathmini na wataalamu, wakulima, wafanya biashara na walaji. Ikionekana inafaa ndiyo inapasishwa.

Ni tofauti kidogo na bidhaa kama vile vinywaji baridi- Kampuni ya Cocacola inapotoa aina mpya ya kinywaji wakati huo inakuwa tayari katika soko. Kwa mbegu za mazao si hivyo. Wanapopasisha mbegu ina maana kuwa mkulima anaweza kuitumia mbegu hiyo kiuzalishaji. Kabla haijapasishwa kama itatumika basi mtaalamu atakuwa hana makosa kama itagundulika kuwa ina hitilafu fulani. Hivyo ndivyo nilivyoelezwa na wataalamu wazalishaji vipando.

TUANGALIE UPYA MAZAO YA BIASHARA


Huku tukiwa tunapata chakula cha mchana hapa Temeke Veterinary (Kwenye makao makuu ya wizara kuu mbili zinazowahudumia wakulima kwa pamoja). Mjadala ulizuka kati yetu wataalamu. Mmoja wetu aliyetembelea wilaya ya Mombo hivi karibuni, alishtushwa na maelezo ya moja ya viongozi wa wilaya hiyo kuwa hawana zao la biashara. Eeh, hamna zao la biashara kabisa? Aliuliza mtaalamu- Ndiyo, alijibiwa. Zamani tulikuwa na zao la mkonge lakini sasa mkonge hauna thamani tena. Tunategemea sana kuuza mpunga huko Moshi, Arusha, Tanga, Morogoro na hata Mombasa, Kenya.
Mtaalamu akahoji tena, mbona mlisema kuwa hamna zao la biashara? Kimya, wakabaki kuchekacheka tu. Na kweli, mtaalamu huyu alitueleza kuwa alipotembelea kwa wanakijiji karibu kila nyumba alikuta nje kumuanikwa mpunga!

Hivi ndivyo tulivyofundishwa na tunavyoendelea kukariri kuwa mazao ya baishara ni pamba, mkonge, kahawa, chai, tumbaku, miwa n.k. hata kama kwenu hamlimi na hujawahi kulitia macho.
Mmoja kati ya wataalamu waliokuwa pale alikiri kwa kusema kuwa hakuwahi kuuona mmea wa kahawa (mbuni) hadi alipoanza kusafiri nje ya kijiji chao.

Baada ya kusema hayo. Labda turudi kwenye mada. Hivi zao la biashara ni lipi? Ukiuza muhogo ukapata fedha siyo zao la biashara kwako? Ukiuza nyanya na ukapata fedha zao hilo siyo la biashara jamani?

Mtazamo wa wale waliotutawala (wakoloni), nadhani ulikuwa ni kwa mazao yale ambayo yaliweza kuuzwa nje kwa faida yao ndiyo waliyoyakubali kuwa mazao ya biashara lakini ndizi hata! Wakati Wachagga, Wahaya, Wanyakyusa wamesomesha watoto kwa biashara ya ndizi sasa haingii akilini mwao kusema kuwa ndizi siyo zao la biashara.
Hata kwenye mfumo wetu wa elimu, kama itatokea swali kwenye mtihani kuwa, chagua zao la biashara kati ya hayo yafuatayo basi kama ndizi lipo na mtoto wa Tukuyu akachagua hilo badala ya pamba atapata bonge la kosa! na pengine kumkosesha kuingia kidato cha kwanza.


Kuna haja ya kuangalia kwa makini mazao ya biashara. Au pengine tusiite ya biashara bali tuyaite mazao yanaoyoingizia taifa fedha za kigeni je seara zetu zinasemaje? Wataalamu wameliona hili.

Tuesday, December 5, 2006

KILIMO NI SAYANSI !

Kazi ya utafiti inafanyika katika vituo vya utafiti na kwenye mashamba ya wakulima. Pichani jopo la wataalamu wa kilimo kutoka Makao Makuu ya Utafiti Dar Es Salaam na kutoka Kanda ya Nyanda za Juu Kusini wakipelemba na kutathmini utafiti zao la mahindi katika kituo cha Utafiti wa Kilimo, Kifyulilo, Mufindi, Iringa (Picha kwa hisani ya ARI-Uyole, Mbeya -Juni, 2006)