Tuesday, November 3, 2009

Vijana wanapaswa kutekeleza kauli mbiu ya KILIMO KWANZA


Ukitembelea katika vijiji vingi hapa nchini hutoshangaa kukuta washiriki wakuu wa kilimo ni wazee. Vijana walio wengi hawajihusishi kabisa na kilimo. Ukiwauliza wanazo sababu nyingi za kutojihusisha na kilimo zilizo nyingi si za msingi. Wakati Taifa linajipanga katika kuitikia kauli mbiu ya KILIMO KWANZA vyema vijana wakaandaliwa ili waifahamu vizuri kauli mbiu hiyo kwa kuwa tayari kwa utekelezaji wake. Kwa hiyo mafunzo mafupi ya uzalishaji wa kilimo yakiandaliwa kwa vijana wetu yatasaidia sana kuboresha uzalishaji wa kilimo. Kilimo kikiachiwa wazee kitakufa.

Tunapoteza shilingi milioni 28 za wakulima kama mchezo


Nimesikitishwa kusoma habari iliyoandikwa kwenye gazeti la Mtanzania la tarehe 2/11/2009 kuwa kiwanda cha sukari cha Ilovo kilichopo Kilombero kimetelekeza miwa ya wanachama 27 wa Chama cha Wakulima wa Miwa katika bonde la Kiliombero yenye thamanin ya shilingi ya Tanzania milioni 28. Habari hii imenistua kwa kweli, kwa umaskini walionao wakulima wetu kupoteza kiasi hicho cha fedha si jambo dogo hata kidogo. Si fahamu ni sababu zipi zilizopelekea uongozi wa kiwanda hicho kukataa miwa hiyo.

Usichelewe kusajili sim card yako


Makampuni ya simu yanayotoa huduma hapa nchini yanaendelea na zoezi la kusajili simu card kwa wateja wake. Blog hii imeshasajili simu card zake za Zain na Vodacom siku ya Jumapili. Zain hawana mlolongo mrefu wa mambo katika kusajili.Tatizo liko kwa Tigo inabidi usote katika foleni. Vipi Tigo ndo tuseme mnawateja wengi? Mimi siamini hata kidogo, hebu boresheni huduma zenu. Banzi wa Moro bado hajasajili simu card yake ya Tigo.

JK amepania kuinua utafiti nchini


Gazeti la Habari leo la tarehe 2 Novemba 2009 limeandika kuwa Rais wa Jamhuri ya Tanzania Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete ameahidi kutoa Tzs milioni 40 kwa ajili ya utafiti wa tufaa (apples) katika kituo cha Utafiti Uyole, Mbeya.

Ni hivi karibuni nimekuwa nikijiuliza kuwa kwanini biashara ya tufaa inaongezeka katika miji yetu wakati sioni wakulima wanaozalisha matunda haya hapa nchini. Jibu ni kwamba tofaa huagizwa kutoka Afrika ya Kusini.

Tanzania zipo sehemu ambazo tofaa zinaweza kuzalishwa kutokana na hali ya hewa ya maeneo hayo sehemu kama vile Lushoto (Tanga), Mgeta (Morogoro) na Mbeya. Iwapo utafiti wa kina utafanyika na kuweza kupata mbegu zinazoweza kustawishwa katika sehemu hizo kutakuwa hakuna sababu tena ya kuagiza tufaa kutoka nje ya nchi, kwahiyo auamuzi wa Mhe. Rais kutoa fedha hizo za utafiti ni chanzo cha kuanza kuzalisha tufaa bora hapa nchini.

HONGERA SIMBA SPORTS CLUB


Mimi ni shabiki wa Club ya Simba au Wekundu wa Msimbazi. Nawapa hongera nyingi wachezaji, coach na viongozi wa klabu kwa ushirikiano mliouonyesha hadi kufanikiwa kuwashinda wapinzani wetu wa jadi Dar Young Africans kwa goli 1-0 uwanja wa Taifa Dar Es Salaam. Mgosi nakupa shavu mdogo wangu!

Saturday, October 24, 2009

Hawakujiandikisha kwasababu mambo ni yaleyale


Uchaguzi wa viongozi wa Serikali za mtaa na vijiji unatarajiwa kufanyika kesho. Wananchi wengi inasemekana kuwa hawakujiandikisha. Ni kweli, Banzi wa Moro katika pitapita yake mjini na vijijini amegundua kuwa watu wamekata tamaa na uongozi wa vijiji na mitaa kwani kasi ya maendeleo hasa huko vijijini ni kidogo sana. Mambo ni yale yale. Viongozi wanaomba nafasi hizo kwa manufaa yao binafsi na wala si ya wananchi. Utasikia ah nikipata nafasi hii baada ya muda wangu wa uongozi kumalizika lazima ninunue 'daladala.'Hivi ndiyo lengo kweli la kugombania uongozi ? Wakati wa kampeni nimeshuhudia vibweka vingi kwa vyama vyote wakishindana kwa rusha roho! Hivi kweli kuna lolote hapa? Ndo maana wengi hawajajiandikisha! (Picha kwa hisani ya gazeti la mwananchi tarehe 24 Oktoba 2009)

Tuesday, October 13, 2009

Mchicha upo wanunuzi je?


Vijana hawa wameamua kuuza mazao ya kilimo hasa mbogamboga. Lakini, wanunuzi wako wapi? Ona mchicha umeanza kunyauka!