Thursday, February 26, 2009

UMEBOBEA KWENYE NINI?

Hebu fikiri mtu anakuuliza hivi mwenzangu ni kitu gani wewe unakifahamu, hakikupatii shida, ni rahisi kukitekeleza bila matatizo. Utasemaje? Tujiulize tumebobea kwenye nini?

TUWE NA TABIA YA KUJISOMEA

Watanzania tulio wengi hatuna tabia ya kujisomea. Hata kwa wasomi wakishapata shahada zao mchezo umekwisha. Ukisafiri kwa ndege, bus, treni, meli ni nadra sana kuwakuta watu wanasoma. Ni wachache utawakuta wameshika angalau gazeti! Lakini ni wazuri kwa porojo tena zisizo na uhakika za kusikia tu, za vijiweni tu. Kwanini tusisome vitabu mbalimbali, majarida mbalimbali? Kama wewe mpenda mpira wa miguu basi angalau uwe unajisomea majarida mbalimbali ya soka. Kama wewe ni mfanya biashara kuna majarida mbalimbali hata kwa kiswahili yanayoelezea biashara.Tukisoma tunajiongezea maarifa. Tunaweza kujenga hoja za msingi tunaweza kuweka mikakati mizuri itakayoweza kutusaidia katika kuboresha maisha yetu. Tusome ili watoto wetu wajifunze kutoka kwetu. Tusilalame na kushuka kwa kiwango cha elimu nchini hata sisi watu wazima hatusomi!

MAENDELEO YAANZIE VIJIJINI

Maendeleo ya kweli ni yale yanayoonekana kwa wengi. Ikiwa vijiji vyetu vitakuwa na huduma muhimu, maji safi, umeme, barabara nzuri, shule, huduma za afya, nyumba bora kwa kweli tutapiga hatua kimaendeleo. Vijana wetu watapenda kuishi vijijini, kufanya kazi vijijini na kuzalisha vijijini. Kwa hiyo nasema Maendeleo yaanzie vijijini.

LIVERPOOL HONGERA!

Mtanzania mimi ni shabiki mkubwa wa SSC. Lakini katika soka la kimataifa ni shabiki mkubwa wa LIVERPOOL ya UINGEREZA. Klabu inayozitoa kamasi vilabu vya Ulaya. Huwa haikati tamaa hata ugenini. Jana imeimaliza REAL MADRID nyumbani kwao 1-0 mbele ya mashabiki wao, katika uwanja wao pamoja na kujaza wachezaji wengi wa kimataifa wenye vipaji. Hongera sana LIVERPOOL.

CUF nao ni walewale

Uchaguzi Mkuu wa Chama cha Wananchi -CUF umekamilika jana. Lipumba-Mwenyekiti na Shariff Hamad-Katibu. Ni wale wale. Maprofessa hawakufurukuta! CUF hawataki mabadiliko.

Sasa wamekuja na panda fedha uvune fedha

Hapa jijini tayari kuna heka heka ya panda fedha! Eti ukipanda milioni moja utavuna milioni moja. Na bila kuongeza fedha kila wakati utakuwa unavuna milioni moja! Wizi mtupu. Watanzania tufanye kazi tusitegemee fedha za bure. Hapo ni mahesabu yanapigwa. Lakini watu hawasikii wanamiminika kama nini wanataka kupanda fedha na kuvuna fedha. Wizi mtupu.

Matrekta pekee hayatoshi kuinua kilimo

Uzalishaji katika kilimo ni matokeo (function) ya mambo mengi ikiwa ni pamoja na teknolojia bora za kilimo, hali ya hewa, rutuba,mbegu bora na elimu ya kilimo kwa wakulima wetu. Pia makongamano, semina, mikutano pia vinahitajika katika kuinua kilimo chetu pamoja na hayo matrekta. Kilimo si matrekta si umwagiliaji si mbolea ...... pekee

Watoto wetu kukosa madawati tulaumiwe wazazi

Nasikitika sana kusoma taarifa kuwa hadi hivi sasa wanafunzi wengi wa shule za msingi na sekondari hawana madawati ya kusomea. Kweli madawati ni ghali lakini tukijiwekea mikakati tunaweza kuwa na madawati kwa watoto wetu. Dawati ni hitaji muhimu kwa mwanafunzi. Hivi Wazazi tunashindwa kuchangia dawati moja kwa watoto wawili kwa miaka saba, au minne? Hata haiwezekani tuanze kuwapatia watoto wetu madawati. Tusingoje maagizo kutoka kwa waziri Mkuu.

Temeke itengeneza barabara ya Kilungule

Wakati mwingine huwa najiuliza kuwa hivi kweli sisi tu wabunifu? Hata kidogo. Mi siamini kama kweli sisi ni wabunifu. Hebu fikiria mwenyewe, Madiwani wa Manispaa ya Temeke, Mkurugenzi na Meya wameshindwa kuweka mikakati ya kuifanya barabara ya Kilungule inayoungana na Yombo hadi Tandika - Davis Corner iweze kupitika wakati wote. Barabara hii ingekamilika ingepunguza kwa kiasi kikubwa matatizo ya usafiri kwa watu wa maeneo ya Mbagala. Juzi nilipita barabara hiyo ni fupi ajabu. Ni dakika 15 kutoka Charambe hadi TAZARA!

Hongera Taifa Stars-Asante Mrisho Ngassa

Juhudi binafsi za mchezaji Mrisho Ngasa ndizo zimetuwezesha watanzania kujidai katika mashindano ya CHAN yanayoendelea huko Ivory Coast . Pamoja na ufupi wake kama mwana blog hii lakini aliruka na kufunga goli la kichwa katikati ya mabeki wa Ivory Coast. Ufupi hoja kwenye kandanda? Alijituma, aliyafanyia kazi maelekezo ya mwalimu na kweli yamelipa. Nakumbuka gazeti moja lilimnukuu kocha Maximo akimweleza Ngassa aache kucheza na jukwaa. Ngassa amezingatia hayo na sasa anafanya maajabu. Kwa bahati nzuri nimeweza kuangalia mechi zote mbili ambazo Stars imekwisha cheza.Kwa kweli Ngassa amekuwa si nyota tu wa Taifa Stars bali nyota wa mechi zote 2. Asante Mrisho Ngassa.

Liyumba kutoroka geresha?

Hivi kweli Liyumba alikuwa na ubavu wa kutoroka? Au geresha? Aende wapi au alikuwa anapima zali?

KILWA ROAD UPDATE 6!

Ndiyo, sasa tumeanza kuichungulia Mtongani kutoka KTM. Uji wa lami unamwagwa na lami inakandamizwa kwa kwenda mbele. KTM -Mbagala Four Ways lami tu. Oh lala!

Tuesday, February 17, 2009

Hatuna ujanja tutapanda Bajaj

Tulijifanya wajanja na kuruka stage ya maendeleo kukimbilia VX. Sasa hatuna ujanja tutapanda Bajaj. Hiyo ndiyo hali halisi. Tulikuwa tunaishi maisha ambayo si yetu!

Mwalimu "nakutiire!"

Hivyo ndivyo alivyoshangaa mwanafunzi kutoka mkoa wa Kagera kwa kuona mwalimu wake akichapwa- Mwalimu "nakutiire."- Mwalimu amechapwa. Nilisikia leo asubuhi kwenye kipindi cha radio moja maarufu hapa jijini. Kweli walimu wetu wamefedheheshwa. Walimu sasa wanachapwa hata na polisi!

Mke wangu ni mwalimu, sijui ingekuwaje kama mke wangu naye angekuwa mmojawao aliyechapwa tena kwa amri ya DC! Tumeshindwa kuwaheshimu walimu hadi kufikia hali hii. Nani atapenda kuwa mwalimu?

Wazaramo hawaachi kucheza ngoma

Baadhi ya Wazaramo wameendelea kudumisha utamaduni wao wa kucheza ngoma kwa muda mrefu. Juma lililopita, blog hii ilishuhudia ngoma iliyochezwa kwa muda wa siku 4 pale kijijini Kisemvule, Mkuranga mkoa wa Pwani. Siku ya Alhamisi shughuli ilianza kwa ngoma ya gombesugu na kumalizia rusha roho ya nguvu siku ya Jumapili. Si sare hizo, si mipasho hiyo, wageni kutoka Dar, mashindano ya kutunzana ndo usiseme. Hao ndiyo Wazaramo hawaachi utamaduni wa kucheza ngoma za kushindana.

KILWA ROAD UPDATE 5!

Imebaki sehemu ndogo tu ya barabara ili wanambagala na vitongoji vyake wateleze!. Sehemu hiyo ni kutoka KTM hadi Mtoni Mtongani. Vingenevyo usafiri wa kwenda Mbagala umeanza kuimarika.

Wednesday, February 4, 2009

Yanga wajitayarishe kuishinda Al Ahly

Ushindi mnono wa mabao 8 dhidi ya timu dhaifu kutoka visiwa vya Ngazija umesafisha njia kwa Yanga kupambana na miambab ya soka barani Afrika - Al Ahly kutoka Misri. Timu hizi kutoka Misri si ngeni kwa Tanzania ukweli ni kwamba timu zetu hupata shida sana kuzifunga timu hizi. Kwa kuzingatia hali halisi hiyo nawataka Yanga wajitayarishe zaidi.

Wanajipima wenyewe na kujiondoa mapema

Huwa sipendi kuwasifia Wamarekani kwa kila kitu, ila kwa hili la kujiondoa mapema wanapojiona kuwa wadhifa wanaopewa unaweza kuwaletea matatizo hapo baadaye Wamarekani wamefanikiwa sana.

Hivi Karibuni Rais Barack Obama aliwateua baadhi ya Wamerikani kushika ngazi za juu katika utawala wake akiwemo Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya na Huduma za Jamii Bw. Tom Doschel ambaye alijiondoa baada ya kuona kuwa alishindwa kulipa kodi ya kiasi cha $ 130,000. Hapa kwetu isingewekana. Kwa hili, Wamerekani nawapa shavu.

Tuesday, February 3, 2009

Benki tatu Mbagala Rangi 3

Ndiyo, huduma ya benki kwa miaka ya hivi karibuni imeongezeka sana katika Manispaa ya Temeke. Pale Mbagala Benki zote tatu maarufu nchini hutoa huduma kwa wananchi wa maeneo ya Mbagala hata wilaya ya Mkuranga na Rufiji. Benki hizo Ni NMB, NBC na CRDB.

Huduma zinazotolewa na Benki hizo kwa ujumla zinaridhisha. Kabla ya kuanza kwa huduma hizo hapo Mbagala wananchi walio wengi walikuwa wanapata huduma hizo Temeke na mjini sasa mambo safi. Kwa mfano kwa Benki ya NBC mara nyingi ATM yake huwa haina foleni kubwa. Kutokana na hali hiyo uwekezaji katika maeneo ya Mbagala unakuwa kwa kasi ya ajabu.

Maghorofa yameanza kuchomoza Mbagala

Kama mchezo vile, maghorofa yameanza kuchomoza hapa na pale maeneo ya Mbagala. Mbagala ya mwaka juzi si ya leo. Wajanja na wanaoona mbali wameanza kuwekeza Mbagala kwa kasi ya hali ya juu. Mbagala sasa inaanza kupendeza.

Tukiwapa motisha askari wetu wa barabarani watadhibiti ajali

Kwa muda wa dakika tano kwa siku ya leo nimeona niandike tena kuhusu ajali kwani ni janga linalostahili kuvaliwa njuga.

Leo asubuhi wakati nikienda kazini nilifurahi kuona magari yakienda kwa mtiririko unaotakiwa kwenye barabara ya Kilwa huwezi kuamini kuwa tulitumia dakika 45 kutoka Kisemvule hadi TAZARA.

Kwanini imekuwa hivyo? Askari wa barabarani na wa FFU ("tigo") walijipanga vyema kwenye sehemu korofi. Kwahiyo hakuna dereva aliyediriki kuchepuka. Matokeo yake usafiri ulikuwa safi na wa salama. Sijui kama askari hawa wamepewa motisha. Lakini naamini kuwa iwapo itapangwa motisha ya aina fulani kwa askari wanaolinda usalama wa barabarani nina uhakika tutapunguza ajali za barabarani na kurahisisha usafiri hapa jijini na kwenye barabaraba zetu za kwenda mikoani.

Biashara ya mchanga kati kati ya barabara!

Kuna mambo mengine yanaendeshwa hapa nchini kama vile hakuna usimamizi, hakuna sheria wala utaratibu wowote.

Wakati huu ambao barabara ya Kilwa inakarabatiwa kuwa ya kisasa zaidi ni ajabu kuona pale Mbagala Zakhem magari makubwa ya kusomba mchanga yakifanya biashara katikati ya barabara. Hivi kweli huu ni utaratibu uliopangwa na Halmashauri ya Manispaa ya Temeke? Hivi kweli viongozi wa Halmashauri ya Manispaa ya Temeke kuanzia madiwani, wabunge na wale wa serikali za mitaa hawajayaona magari haya? Magari haya ni moja ya kero ya usafiri kwa wakazi wa Mbagala. Hivi kwenye vikao vya madiwani huwa kinazungumzwa nini? Biashara hii ikome.

Albino na Ajali za barabarani ni majanga yanayotumaliza

Jana jioni wakati natoka kazini kurudi nyumbani kwangu Kisemvule kwa kupitia barabara ya Kilwa, pale Mwandege kulitokea ajali mbaya iliyohusisha bus ndogo za abiria na shangingi moja (nasikia ni mali ya mahakama). Habari nilizozipata ni kwamba watu watatu walifariki papo hapo na wengine kuumia vibaya.

Ajali hizi za mara kwa mara zinaongezeka siku hadi siku.Watu wanapoteza maisha lakini mambo ni yale yale. Gari zina kwenda mwendo wa kasi bila sababu ya msingi. Katika kipindi cha mwezi mmoja kwenye barabara hiyo kumetoka si chini ya ajali 10 na kupoteza maisha si chini ya watu 10.

Hivi kweli tumeshindwa kudhibiti ajali za barabarani? Mimi naona inawezekana kabisa. Sheria za barabarani zipo zifuatwe. Magari yakaguliwe na anayekosa apate adhabu kali bila ya kuwapa muda wa kuzungumza au kumuona fulani ili kesi idhoofishwe. Ajali za barabarani ni kama mauaji ya Albino zinatumaliza Watanzania. Tutaogopa kupanda magari!

Monday, February 2, 2009

Tunapenda kula wali lakini........!

Jumamosi na hata siku ya Jumapili (jana) blog hii ilifanya kazi kwenye plot ya mpunga. Kwa shughuli za kupanda na kupandikiza.

Jamani lazima niseme ukweli kilimo cha mpunga ni shughuli pevu. Shughuli ya kupanda na kupandikiza ni shughuli ngumu sana. Sasa ninafahamu kwanini bei ya mchele ni kubwa sana kuliko mahindi. Kustawisha mpunga ni kazi. Nawapongeza wakulima wa mpunga. Nimejifunza kuwa kama kweli Tanzania tumedhamiria kuinua uzalishaji wa mazao ya kilimo inatubidi kuwekeza kwa kiasi cha kutosha kwenye kilimo.

Tuwekeze kwenye zana ili zirahisishe kazi ya shambani, tuwekeze kwenye mbegu bora ili tuweze kuvuna mpunga mwingi na mzuri, tuwekeze kwenye pembejeo nyingine kama vile madawa na mbolea vinginevyo uzalishaji utaendelea kuwa mdogo mwaka hadi mwaka na hivyo kufanya mpunga kuwa mchache sokoni matokeo yake ni kupanda kwa bei ya mchele. Uzalishaji unapokuwa mdogo na mahitaji makubwa ni dhahiri bei itapanda tu.

Tshs 440,000/= faida ya karanga kwa Hekta

Wakulima wanapaswa kufahamu mapato yanayopatikana katika uzalishaji wa mazao mbalimbali. Katika tafiti zao watafiti wa kituo cha Utafiti Naliendele-Mtwara wanasema kuwa, ukitoa gharama zote za uzalishaji wa karanga kwa hekta na kwa kutumia bei za mwaka 2007/08. Mkulima ana uhakika wa kupata faida ya Tshs 440,000/= kwa hekta.

Ufuta unalipa

Watafiti wa ufuta wanasema ukitumia teknolojia bora kwa kulima ufuta unaweza kupata Tshs 352,500/= kwa hekta moja baada ya kutoa gharama zote.

NAMI NALIA NA PINDA

Kauli aliyoitoa Pinda kuhusu mauaji ya kinyama wanaofanyiwa ndugu zetu Albino ni kauli ya uchungu ni kauli inayoonyesha kuwa Serikali haitowavumilia wauaji hao wanapokutwa wakifanya tendo hilo. Hakuwa na maana kuwa mtu akituhumiwa auawe. Lakini akithibitika bila kuhoji basi nao wanastahili adhabu "kama hiyo."

Hivi sisi Watanzania tukoje? Mtu anaua, mtu anawakosesha raha watu wenzake halafu mnasema sheria sheria! Ah bwana kwa hili mimi nalia na Pinda wauwawe tu basi. Labda hayajakufika. Baba yako anauawa kinyama, mtoto wako, mke wako mama yako dada yako. Halafu wengine wanaleta siasa. Mimi nikumkuta nachinja!

Waziri Mkuu alilia kwa kuwa anajua ukubwa wa tatizo hilo. Tulie pamoja na Pinda

KILWA ROAD UPDATE 4!

Matengenezo ya barabara ya Kilwa ( Mto Mtongani-Mbagala R3) yanaendelea vizuri licha ya mvua zinazonyesha kwa sasa kiasi cha kupunguza kasi ya utengenezaji wa baraba hiyo. Juma la jana Blog hii imeshahudia uwekaji wa lami kwenye keepleft ya Kizuiani pamoja na uwekaji wa lami kutoka St.Anthony Sekondari hadi sabasaba.

Tatizo kubwa ni kwa madereva wenye haraka wasiopenda kufuata utaratibu na kusababisha msongamano usio wa lazima hasa nyakati za asubuhi na jioni. Vinginevyo barabara inasonga mbele nina matumaini makubwa kuwa ifikapo mwezi watatu (Machi) usafiri wa Mbagala utakuwa bomba n tayari tumeshaanza kuyaona mabus mazuri yakija Mbagala!