Tuesday, January 16, 2007

PAMOJA NA KUONDOA WAMACHINGA-Dar bado chafu

Jumapili iliyopita nilitembelea Kariakoo, Ilala, Tandika, Mbagala na Temeke.
Tusidanganyane, Dar bado chafu. Kila nilipopita malundo ya taka yamejaa kibaa kando ya barabara kuu, uchochoroni, nyumba za watu na wakati mwingine hospitalini!

Pale kwenye maghorofa ya nyumba za "NHC" Ilala, maji taka yanatiririka hovyo, hovyo inabidi uwe mtaalamu wa kuruka viunzi ili usiyakanyage na kama umevaa ndala ndiyo hakuna pa kukwepa utakanyaga tu.

Haya, pale karibu kabisa na Hospitali ya Manispaa ya Temeke pale nje, karatasi kibao, nyingine ziko kwenye mifereji ya maji machafu.

Kule Tandika sokoni mambo ni yale yale, uchafu, uchafu, uchafu mpaka mtaa wa Bubu wote kuchafu!

Mtoni Mtongani karibu kabisa ya kituo cha mabasi ya daladala kuna lundo la uchafu na kibaya zaidi watu wanachakurachakura wakiokoteza vinavyowafaa na watu wanaangalia tu.

Nakutana na magari ya kuzoa uchafu, he, kichekesho. Mengine hayana taa za mbele yamechakaa choka mbaya lakini yanapita barabarani. Hivi kweli kuna sheria inayoruhusu magari ya kubeba uchafu yawe machakavu pia? Askari wa usalama barabarani wanaona hilo wanafumbia macho wao kazi yao kukamua magari ya mkaa na daladala. Ukikutana na magari hayo ziba pua. Hiyo harufu! Kibaya yanasomba uchafu na kudondosha uchafu barabarani.

Dar bado chafu, hata pale Kariakoo mitaa karibu yote ni michafu, nenda Tandamti, Sikukuu, Kongo, na Aggrey ni michafu.

Mimi najiuliza, tumewaondoa wamachinga sawa. Lakini mbona Jiji bado chafu? Hivi itachukua muda gani kuona "impact" ya kuwaondoa wamachinga hasa kwenye suala la usafi?

No comments: