Tuesday, January 9, 2007

NIMERUDI KUTOKA MATOMBO!

HERI YA MWAKA MPYA!

Ndiyo, nimerudi kutoka Matombo. Matombo ya mwaka 2006, siyo ya 1970s.
Matombo ya sasa mambo kwa fedha tu. Huna sababu ya kubeba sukari kutoka Moro au Dar, huna sababu ya kununua khanga au kitenge kutoka Dar au Moro huna sababu ya kubeba bia wala soda. Mambo yote Matombo tu.

Matombo kumekucha, Matombo kumebadilika. Matombo mtandao wa Celtel unatamba huku nayo TTCL baba wa mawasiliano akionyesha kali yake.

Matombo sasa mambo kwa Solar kama si solar basi "generator" lakini siyo za Richmond! Watu wanaona TV, humdanganyi mtu. Ndiyo, hata World Cup mbona wenzio waliona "live." Unashangaa nini sasa?

Matombo bado ukarimu uko pale pale. Natoa zawadi ya thamani ya shilingi elfu mbili. Napata jogoo mkubwaa. Kila siku kuku tu. We acha tu. Kila siku ndizi, maembe, ubwabwa, mashelisheli, mafenesi, mananasi ni tafrija tupu!

Matombo imebadilika. Vijana wanaongelea kulima kitaalamu. Nakutana na Michael Mloka Tunywe, ananitembeza kwenye bustani yake aliyopanda migomba, minazi, minanasi, midimu natembea hadi nachoka baadaye ananiomba ushauri afanye nini?Lakini soko hakuna nanasi hadi shilingi mia moja unapata. Namshauri. Kweli inatia moyo.

Mfizigo nayo je bado ipo? Ah bado. Kijiji kimepiga marufuku uchimbaji wa madini kiholela bila kuzingatia hifadhi ya mazingira. Big up wazee wangu. Nilienda kupiga "solono" nikateleza, vidonda nimerudi navyo na kuvitibu pale St. Vincent Dispensary, Vikindu kwa masista-wakaniambia pole sana.

Matombo kumekucha, vijana wanajenga nyumba bora kwa kutumia matofali ya kuchoma na kuezeka kwa mabati. Kijiji cha Lumala kinatia fora, sasa mambo yanaelekea Utunu, Mng'ombe hadi Nyangala! Kiswira, Nige, Gubi, Mhangazi bati pweya!

Kanisani je. Kwaya ya Mtamba inaendelea kutia fora. Ndiyo waliopangiwa kuimba usiku wa Christmass. Walikuja kwa mbwembwe kwa kukodi Costa wakiimba kwa mbwembwe huku wakipambwa na T-SHIRT zenye nembo ya kanisa la Mt.Paul Matombo. Kanisa nililobatizwa, kupata Komunio hata Kipaimara. Hapa ndipo nilipotumikia kanisani katika ibada za misa takatifu.

Kiswira, hapa ndipo kwetu hapa ndipo nilipopata elimu yangu ya msingi. Makao Makuu ya klabu ya Mpira ya Kiswira. Klabu ambayo tuliijenga sisi wenyewe kwa kubeba matofali moja moja hata kama ni mdogo kiasi gani na kusaidiwa na Brother Rudolph aliyekuwa kiongozi wa kiwanda cha Mayungi kilichozalisha mafundi seremala wengi kutoka Matombo. Nguvu ya Kiwanda hicho ni kutoka kwenye maporomoko ya Mayungi. Nasikia maporomoko hayo yanaweza kuzalisha umeme wakutosha na kulisha tarafa nzima ya Matombo!

Watu wanakalia taarifa, tunategemea Richmond hadi Matombo ?Hatutofika!

No comments: