Thursday, December 21, 2006

NI KWELI HALMASHAURI ZA WILAYA ZINAPOTEZA MAPATO

LEO asubuhi nikiwa kwenye bus litokalo Mkuranga kwenda Mbagala, tulipofika Vikindu (Kwenye kizuizi cha kukagua mazao, madini, na raslimali nyingine). Kuna abiria aliyekuwa na mzigo wa kulipia ushuru sifahamu ni mzigo gani. Basi watoza ushuru hao wa Vikindu walimwambia alipe Tshs 900/= abiria huyo alitoa chapchap wala bila kudai stakabadhi ya malipo na gari hilo likaondoka!

Kwa hakika nilimuona mtoza ushuru yule akiweka noti ya Tshs 500/= kwenye shati lake. Nikajiuliza ni kiasi gani cha mapato kinapotea kwa njia hii? Ni mamilioni. Hatuwezi kuendelea kwa njia hii. Ni hatari, hakuna usimamizi mzuri pale. Na hii ni kwa Vikindu tu. Je kuna vituo vingapi vya aina hii vinavyopoteza mapato kirahisi rahisi tu nchi nzima?

Lakini tatizo liko kwa walipaji, wao wanafikiri aa shs 900 tu mbona kidogo! Je, kwa mwezi wakitokea watu 20,000 ambao hawakupewa stakabadhi ya malipo. Halmshauri ya Mkuranga kwa kizuizi cha Vikindu kitakuwa limepoteza milioni 18! Si haba. Ni madarasa mangapi hayo ya shule ya msingi yangejengwa kwa mwezi, kwa fedha za Vikindu tu? Tuwe makini.

Tuna uwezo wa kuendelea, tatizo ni sisi wenyewe.

Chrsitmass njema.

Nitakuwa Matombo, Morogoro kwa muda wa majuma mawili. Naenda kula "mwidu" na "komola."

No comments: