Tuesday, December 5, 2006

TUWE MAKINI KATIKA KUTOA HUDUMA

Jana mchana nikiwa pale TAZARA-Station nikipata chakula cha mchana. Labda niseme wazi chips na mishkaki, nilibahatika kukaa meza moja na kijana mmoja mtanashati naye akisubiri kupata mlo. Kwa bahati mbaya huduma ilikuwa si nzuri. Ilichukua karibu dakika 30 kupatiwa nilichooagiza. Naye yule kijana aliagiza soda lakini sprite, jinsi alivyojibiwa na muhudumu inasikitisha. Basi hapo ndipo tulipoanza kujadili kama kweli wahudumu wale wanajua wanachokifanya. Lakini tulikuja kugundua kuwa wenzetu walioagiza ugali na wali huduma waliipata chapchap. Kumbe kwenye kibanda kimoja watoa huduma ni tofauti. Kuna anayemiliki kibanda cha chips na kuna anayemiliki "ubwabwa" Kwa kweli inasikitisha sana. Itakuwaje mtu usubiri chakula muda wa nusu saa wakati pale si hotelini?

Tatizo hili la utoaji huduma hapa Tanzania kwa kweli limeshakuwa kero. Unakwenda Benki kuweka fedha au kuchukua fedha huduma ni goigoi. Ukiuliza, majibu unayopata kwa kweli yanakatisha tamaa. Unakwenda kulipa bill ya umeme unakuta dirisha la kupokelea fedha limefungwa. Unaenda kununua nyanya sokoni, muuzaji anakufokea. Umeamua kupunzika na familia yako kwa kupata kinywaji, wahudumu baada ya kuona una familia hasa mke wako basi ndiyo kabisa umewafukuza wako kuleee. Jamani kwa mtindo huu kweli tutajiajiri? Inalipa kweli kwa biashara hii. Mtu anakuletea fedha, wewe unamkatisha tamaa. Eti unasubiri mteja aanze kuuliza badala ya wewe mtoa huduma kumkaribisha vizuri na kumwelekeza. Labda niwe muwazi kidogo, hapa Tanzania kama biashara inaendeshwa na wenzetu Wachagga utaona tofauti kubwa sana. Huduma nzuri. Kma ni mahali pa chakula patakuwa pasafi, wahudumu watatoa huduma nzuri na uzimamizi mzuri. (Nimekuja kutafuta pesa msee! Atakwambia Mchagga). Lakini waswahili ndiyo hivyo tena. Yule kijana alinieleza, kule Tanga ni balaa maana huduma zinatolewa taratiiibu hawana haraka (Wajaleo.......). Kama tunataka kujiajiri lazima tubadilike katika utoaji huduma lasivyo tutabadilishwa na fedha tutazikosana na tutabaki tulivyo . Kwa mwendo huu wa kusubiri chips dakika 30 mimi nimeshindwa!

No comments: