Tuesday, December 12, 2006

HIVI NI KWELI MIAKA 45 YA UHURU SEKTA YA KILIMO HAIJAFANYA LOLOTE?

Siamini kuwa miaka 45 tangu tupate UHURU wetu hakuna mafanikio kwenye sekta ya kilimo. Mafanikio yametajwa tu kwenye Elimu, Ujenzi wa Barabara kwa sababu ni rahisi kupima! Tusiwe wavivu jamani. Kweli hakuna viashiria kwenye sekta ya kilimo vinavyoonyesha mafanikio?

Imekuwa ni desturi sasa kuwa kila inapotayarishwa taarifa ya nchi hasa inapohusu mambo chanya, sekta ya Kilimo (mazao na mifugo) haimo. Ikumbukwe kuwa sekta hii inaajiri asilimia 80 ya watanzania na kulisha asilimia 100 ya watanzania sasa inawezekana vipi kutokuwa na mafanikio.

Kuna tatizo. Tatizo lipo kwa wale wanaokusanya taarifa na kuzitayarisha. Huenda hawajishughulishi kuweza kufahamu Kilimo imefanya nini. Mimi nina uhakika kuwa Kilimo imefanya mambo mengi kwenye masuala ya utafiti, umwagiliaji na mafunzo ukilinganisha kabla ya kupata uhuru. Hata uzalishaji umeongezeka pia kwa baadhi ya mazao na kuna mazao ambayo sasa yana umuhimu mkubwa katika taifa kuliko ilivyokuwa hapo awali(Kabla ya UHURU) uzalishaji wa maua ambao umeliingizia taifa fedha nyingi za kigeni. Lakini waliomwandikia Rais wetu mafanikio ya nchi miaka 45 baada ya UHURU wamepuuza hayo. Nchi imewekeza fedha nyingi sana kwenye sekta hiyo haiwezekanai kutokuwa na mafanikio. Unapozungumzia vyuo vikuu. Kwanini usiseme kuwa kuna Chuo Kikuu cha Sokoine ambacho kinatoa taaluma za sayansi ya kilimo ambapo kabla ya UHURU hatukuwa nacho. Huko unaweza kupata wataalamu wa Kilimo waliozalishwa na chuo hicho ambao wanafanya kazi ndani na nje ya nchi. Je, hayo siyo mafanikio ya nchi katika sekta ya Kilimo? Kuna mengi. Tusiwe wavivu katika kutayarisha taarifa.

No comments: