Thursday, December 7, 2006

HATUJAMFIKIA MKULIMA -WASSIRA

Waziri wa Kilimo Chakula na Ushirika Mh. Stephen Wassira amesema bayana kuwa wafanyakazi wa kilimo bado hawajamfikia mkulima. Mh.Wassira aliyasema hayo alipokutana kwa mara ya kwanza na wafanyakazi wa Wizara hiyo walioko Makao Makuu - Temeke Veterinary, tarehe 1/12/2006, Ijumaa.

Akiongea na wafanyakazi hao kwa muda usiozidi dakika 15. Waziri Wassira alisema kuwa, Wizara ina majukumu makuu mawili (1). Inatoa ajira kwa asilimia 80 ya Watanzania (2). Inawajibika kuhakikisha kuwa asilimia 100 ya watanzania wanapata chakula cha kutosha wakati wote.

Waziri alitoa changamoto kwa wafanyakazi hao kwa
- kumfikia mkulima kijijini ili aweze kupata mapato halisi kutokana na kilimo
- kufanya kila linalowezekana ili kuhakikisha kuwa watanzania wanapata chakula.

Aliwashauri wafanyakazi wote kuchapa kazi na kusema kuwa hakuna kazi isiyokuwa na maana na mshahara anaolipwa kwa kila mfanyakazi ni gharama kwa hiyo ni lazima kufanya kazi kwa pamoja ili Wizara iweze kutimiza malengo yake.

Kabla ya kuanza mazungumzo na wafanyakazi hao, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Mh. Peniel Lyimo alitoa taarifa kwa Waziri kuwa, Wizara ina jumla ya wafanyakazi 2,600. Kati ya hao wafanyakazi 1,165 wako kwenye Idara ya Utafiti na Mafunzo. Ni wafanyakazi 400 tu ndiyo wanaofanya kazi Makao Makuu ya Wizara.

Kikao hicho cha muda Mfupi kilihudhuriwa pia na Naibu Waziri wa Kilimo na Chakula Mh. Dr. David Matayo David na Naibu Katibu Mkuu Mh. Mohamed Muya.

Hii ni mara ya tatu kwa Waziri Wassira kuiongoza wizara hiyo. Mwaka 1973 aliteuliwa kuwa Naibu Waziri , Wizara ya Kilimo akiwa na umri wa miaka 27. Mwaka 1989 alirudi tena kwenye Wizara hiyo akiwa Waziri na mwaka huu mwezi Oktoba Rais Jakaya Mrisho Kikwete amempa jukumu la kuiongoza wizara hiyo.

No comments: