Wednesday, December 20, 2006

KWAHERI NATHANIEL KATINILA

Msiba mkubwa umetupata Wizara ya Kilimo Chakula na Ushirika, Ofisi ya Waziri Mkuu na Programu ya Kuendeleza Masoko ya Kilimo (AMSDP) kwa kuondokewa na mmoja kati ya vijana waliobobea katika fani ya kilimo naye si mwingine bali ni Marehemu Nathaniel Katinila (45) juma lililopita. Marehemu alifariki kwa ajali ya Ndege Cessna 5HTZ mali ya Tanzair iliyotokea Mbeya tarehe 16/12/2006.

Mimi namfahamu sana Katinila. Mwaka 1981 tulikutana pale MATI- Ukiriguru mimi nikiwa mwaka wa pili (DIP - CROP PRODUCTION) naye akiwa amekuja kuanza kozi hiyo hiyo. Baada ya kuhitimu masomo yake akafanya kazi miaka michache (sifahamu ni sehemu gani) baadaye akajiunga na Chuo Kikuu cha Sokoine ambako alipata shahada yake ya kwanza yenye mchepuo wa Uchumi Kilimo. Tulikutana tena mwaka 1993 katika Wizara ya Kilimo na Mifugo, Idara ya Utafiti na Mafunzo, yeye akiwa ARI-Naliendele Mtwara nami nikiwa Makao Makuu Dar Es Salaam wote tukiwa wachumi kilimo mwenzangu "Kati" (Nilizoea kumwita hivyo) akiwa kwenye programu ya "Farming Systems Research and Socio-Economics" nami nikiwa kwenye Kitengo cha Mipango, Kupelemba na Kutathmini (Planning, Monitoring and Evaluation).

Tukiwa pale Ukiriguru, wote tulishiriki kwenye kikundi cha maigizo kilichojulikana kama "MAJOSA" chini ya mwalimu wetu Benito Mwenda ambaye alikuwa mwanachuo mwenzetu ingawa kwa sasa ni Mkufunzi hapo hapo MATIU. Tukiwa chuoni Katinila alikuwa pia "Boxer."

Akiwa Naliendele amefanya kazi nyingi za utafiti katika masuala ya farming systems. Baadaye alijiunga na mradi wa " RIPS" uliokuwa ukiendeshwa mikoa ya kusini kabla ya kurudi tena Kilimo pale Naliendele.

Mara tu ilipoanzishwa Programu ya Kuendeleza Masoko ya Kilimo. Nathaniel alibahatika kuwa Mratibu wake wa Kwanza.

Namfahamu sana Katinila kwa mema yake kuliko mabaya. Alikuwa mshauri mzuri, mpole na asiye na pupa. MUNGU AIWEKE MAHALI PEMA PEPONI ROHO YA NATHANIEL KATINILA. AMINA.

No comments: