Thursday, December 7, 2006

TUANGALIE UPYA MAZAO YA BIASHARA


Huku tukiwa tunapata chakula cha mchana hapa Temeke Veterinary (Kwenye makao makuu ya wizara kuu mbili zinazowahudumia wakulima kwa pamoja). Mjadala ulizuka kati yetu wataalamu. Mmoja wetu aliyetembelea wilaya ya Mombo hivi karibuni, alishtushwa na maelezo ya moja ya viongozi wa wilaya hiyo kuwa hawana zao la biashara. Eeh, hamna zao la biashara kabisa? Aliuliza mtaalamu- Ndiyo, alijibiwa. Zamani tulikuwa na zao la mkonge lakini sasa mkonge hauna thamani tena. Tunategemea sana kuuza mpunga huko Moshi, Arusha, Tanga, Morogoro na hata Mombasa, Kenya.
Mtaalamu akahoji tena, mbona mlisema kuwa hamna zao la biashara? Kimya, wakabaki kuchekacheka tu. Na kweli, mtaalamu huyu alitueleza kuwa alipotembelea kwa wanakijiji karibu kila nyumba alikuta nje kumuanikwa mpunga!

Hivi ndivyo tulivyofundishwa na tunavyoendelea kukariri kuwa mazao ya baishara ni pamba, mkonge, kahawa, chai, tumbaku, miwa n.k. hata kama kwenu hamlimi na hujawahi kulitia macho.
Mmoja kati ya wataalamu waliokuwa pale alikiri kwa kusema kuwa hakuwahi kuuona mmea wa kahawa (mbuni) hadi alipoanza kusafiri nje ya kijiji chao.

Baada ya kusema hayo. Labda turudi kwenye mada. Hivi zao la biashara ni lipi? Ukiuza muhogo ukapata fedha siyo zao la biashara kwako? Ukiuza nyanya na ukapata fedha zao hilo siyo la biashara jamani?

Mtazamo wa wale waliotutawala (wakoloni), nadhani ulikuwa ni kwa mazao yale ambayo yaliweza kuuzwa nje kwa faida yao ndiyo waliyoyakubali kuwa mazao ya biashara lakini ndizi hata! Wakati Wachagga, Wahaya, Wanyakyusa wamesomesha watoto kwa biashara ya ndizi sasa haingii akilini mwao kusema kuwa ndizi siyo zao la biashara.
Hata kwenye mfumo wetu wa elimu, kama itatokea swali kwenye mtihani kuwa, chagua zao la biashara kati ya hayo yafuatayo basi kama ndizi lipo na mtoto wa Tukuyu akachagua hilo badala ya pamba atapata bonge la kosa! na pengine kumkosesha kuingia kidato cha kwanza.


Kuna haja ya kuangalia kwa makini mazao ya biashara. Au pengine tusiite ya biashara bali tuyaite mazao yanaoyoingizia taifa fedha za kigeni je seara zetu zinasemaje? Wataalamu wameliona hili.

No comments: