Tuesday, January 16, 2007

TUNANAKILI HATA MAJINA!

Enyi Watanzania wenzangu, leo nimeamua kuandika kuhusu tabia iliyozuka kwa baadhi yetu ya kutaka kunakili kila kitu (copying). Kibaya zaidi tunanakili hata majina!

Hebu fikiria mtu anaanzisha shule ya sekondari, pamoja na gharama zote alizogharamia, baadaye anaiita St. Mary's au St. Mathew. Hivi ndani ya vichwa vyetu kuna nini? Kuna ulazima wowote wa kuita Saint, Saint.

Na sisi wazazi tukiona shule inaitwa St.... basi vichwa juu. Mimi nitampeleka mtoto wangu St. Elizabeth, mwingine St. Anne, mwingine St.Luka. Hivi kuna siri gani na shule hizi zinazoanzia na St? Wizara inayohusika ilijibu hili. Pengine hizi hazilipi kodi au zinapoingiza vifaa vya shule huwa hazitozwi ushuru maana ni za watakatifu hizi!

Natumaini wengi wenu mtakubaliana nami kwamba miaka kumi iliyopita upuuzi kama huu haukuwepo. Wengine tumesoma Njombe Sekondari, Tosamaganga Sekondari, Ilboru Sekondari, Tambaza Sekondari, Kilakala Sekondari, Loleza Sekondari, Mkwawa Sekondari, Iyunga Sekondari . Hata Mh. Rais Jakaya Mrisho Kikwete amesoma Kibaha Sekondari. Shule zilikuwa nzuri tu, wanafunzi walikuwa wanafaulu vizuri tu. Tena ilikuwa fahari kusema mimi nasoma Tosamaganga Sekondari. Lakini siku hizi shule hizi zinazoitwa za binafsi na majina nayo yabinafsi kweli utasikia shule inaitwa California nyingine Mississippi mh hapa ndo tumefika. Au shule hizi zinapata misaada kutoka ng'ambo kama tulivyozoea? Misaada, misaada, misaada hata vyoo misaada kutoka Japan na wafadhili wanaweza kusema jina la choo kiitwe.......... maana ni msaada!

Shule umeijenga mwenyewe, kwanini usiite Shule ya Sekondari Jambuya?. Maana unajua maana yake, pengine Jambuya ni jina la babu yako utakuwa umemuenzi babu yako na kwakweli pengine dunia nzima kutakuwa na shule hiyo tu yenye jina hilo. "that is unique".

Ikiwa hata majina tunanakili tunachokiweza hasa ni kipi? Hebu wenzangu mnieleze. Wanaohusika hawajaliona hili au nao ndiyo wale washabiki wa St au California?

Tufikiri upya.

No comments: