Thursday, June 26, 2008

Ingekuwa si Bajaj?

Nilipokwenda Tegeta kumtembelea rafiki yangu Phillip na kuhudhuria sherehe za kommunio ya mwanae Kenny nilitumia Bajaj, juzi nilipotembelea Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Mikocheni nilitumia Bajaj kutoka Mwenge hadi hapo kituoni. Jana nilikuwa na shughuli za kikazi huko Mikocheni - Maabara ya TFNC (Chakula na Lishe) nilifika huko kwa kutumia Bajaj.

Bajaj ni aina ya chombo cha usafiri mfano wa pikipiki yenye magurudumu matatu. Usafiri huu umeanza kuenea kwa kasi kubwa hapa jijini Dar Es Salaam hasa kwa zile sehemu ambazo usafiri wa daladala haupo na barabara ni mbaya au ni nyembamba sana. Licha ya kupata upinzani mkali kutoka kwa madereva wanaondesha taxi, lakini wenye maamuzi ya kutumia au kutotumia bajaj ni wateja.

Kwanini wateja wanapenda Bajaj?
  • Bei poa ukilinganisha na taxi
  • Abiria hawazidi watatu na wote wanakaa kwenye kiti
  • Hupita kwenye barabara zilizoshindikana
  • Hazina mwendo wa kasi
  • Zinakufikisha mahali unapotaka
  • Haipotezi muda ikiwa na wateja

Nilipojaribu kumdadisi dereva mmoja wa bajaj kuona kama inalipa. Alisema " Bajaj inalipa sana Mzee." Kwa Siku yeye hupeleka Tshs 15,000/= kwa mwenye mali. Kama mambo yakienda vizuri baada ya miezi 7 inaweza kurudisha gharama za manunuzi (Kwa sasa Bajaj 1 ni Tshs 4,000,000/= sina uhakika).

Hiyo ndiyo Bajaj iliyoanza kwa shida na sasa kutapakaa Tegeta, njia panda ya White Sands, Mwenge, Kawe na kwingineko jijini Dar. Na kwakweli zinatoa huduma ya kuridhisha kwa wasafiri wa sehemu hizo. Hata hivyo nadhani bado kuna uwanja wa kuboresha huduma hii ya usafiri. Unasemaje kuhusu Bajaj?

1 comment:

Belo said...

Jamaa wa Bajaj wameua kabisa soko la teksi hasa maeneo ya Mwenge,Tegeta,Mikocheni
Jamaa wa teksi wakiona Bajaj wanzigonga na hawasimami kwani wameua soko lao
Siku hizi hakuna wa kupanda teksi hata kama ni usiku au kama una mabegi yote yanakaa kwenye bajaj