Friday, September 18, 2009

Enzi zangu Njombe Sekondari


Mwaka 1974 niliitwa 'Bazooka' 'Mugia' pale Njombe Secondary School (NJOSS). Nilikuwa mmoja kati ya wanafunzi wadogo pale shuleni si kwa ufupi tu hata kwa umri. Namkumbuka mtoto mwingine alikuwa ni Morris Calist (Mchaga) na mwingine tena Mchagga (jina nimesahau). Wenyeji wa Njombe mjini walikuwa wakitushangaa sana kuona watoto wadogo tukisoma sekondari - wenyewe wakituita 'wasekondari.'

Wakati ule shule hii ilikuwa maarufu sana wilaya nzima sekondari moja tu. Tukigoma mkuu wa wilaya anatusikia! Tulikuwa tunapata miche ya sabuni, Tanbond na karanga, chai kwa mikate (virungu), magodoro hapohapo shuleni, madaftari bure! Isitoshe tukifunga shule mabasi ya 'Railways' yalikuwa yakitusafirisha hadi nyumbani kwetu serikali inalipa. Mimi yalinifikisha hadi Magomeni Qtrs. Nakumbuka yalikuwa yanapitia barabara ya Kondoa pale Magomeni tulikuwa na akina Michael Luanda, Lawrence Mkude. Wote tulikuwa sawa hakuna tajiri wala maskini! Shuleni hapo darasa moja tulikuwa na Henry Aikael Mbowe (Kaka yake Philemon Mbowe-Mwenyekiti wa Chadema).Nyumbani tuliitwa 'WASEKO.' Sasa mambo yamebadilika kabisa wanaosoma shule za sekondari za serikali wanadharauliwa eti wanasema shule za kata ni shule za walala hoi.Mtoto akichaguliwa kwenda shule ya serikali wazazi wanamuhamisha wanampeleka 'Private.' Pichani Banzi wa Moro akiwa NJOSS nje ya Maktba ya shule mwaka 1974.

No comments: