Monday, December 29, 2008

Banda la Kumpuzika wasafiri lijengwe Msalabani

Kwa wenyeji wa Matombo au waliobahatika kufika Matombo, jina MSALABANI si geni ni jina maarufu. Hapa ndipo ilipo njia panda ya kwenda Matombo Mission, Tawa, Konde, Nyingwa, Kibungo, Lukenge, Nyangala na vitongoji vingine vya Matombo.

Vitongoji hivi vina wakazi wengi ambao kwa usafiri wa uhakika inawabidi kusafiri hadi Msalabani ambapo ndipo kwenye barabara kuu itokayo Morogoro kwenda Kisaki. Tatizo la mahali hapa ni ukosefu wa Kibanda cha kupumzika abiria.

Juzi Jumamosi wakati nasafiri kuelekea Morogoro mjini abiria wengi tulinyeshewa na mvua na kulowa chapachapa. Wanawake ilibidi wabadilishe nguo zao hapohapo baada ya kukatika kwa mvua.

Hivi uongozi wa Matombo hawaoni umuhimu wa kujenga kibanda imara japo kilichoezekwa kwa makuti ili kuwahifadhi abiria wakati wa jua au mvua? Hili linawezekana. Tuanze sasa kabla ya masika.