Monday, August 4, 2008

Zongo Mwenyekiti Lugaluga Agricultural and Marketing Cooperative Society

Mkutano Mkuu wa Ushirika wa Kilimo na Masoko - Lugaluga (Lugaluga Agricultural and Marketing Cooperative Society) uliofanyika tarehe 2 Agosti 2008 kwa kauli moja umepitisha jina la Bw. Ally Rashid Zongo kuwa Mwenyekiti mpya wa chama hicho baada ya aliyekuwa Mwenyekiti wa ushirka huo Bw. Chaula kuhamia Mbeya kikazi.

Kabla ya hapo Bw. Zongo alikwa akishika nafasi ya Makamu wa Mwenyekiti katika Ushirika huo. Kwa maana hiyo, Bw. Zongo ndiye Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Ushirika huo.

Chama cha Ushirika wa Kilimo na Masoko Lugaluga kilichopo Morogoro kilisajiliwa rasmi Septemba 2005 na kupewa namba 344. Hadi sasa ushirika una wanachama 88 wanaotimiza masharti na kanuni za chama.

Ushirika wa Lugaluga una mpango kabambe wa kumiliki ekari 20,000 zitakazotumiwa na wanachama wake katika uzalishaji wa kilimo na ufugaji.

Dira ya Lugaluga ni kuinua na kustawisha hali ya uchumi na maisha ya wanachama na jamii kupitia vyama vya ushirika.

Lugaluga ni chama chenye kuona mbalimbali katika uzalishaji wa kilimo na ushirika.
Pamoja na raslimali kubwa ya ardhi iliyoko mbele yao, Lugaluga inakosa mtaji wa kujiendesha.

Kwa kuwa mkoa wa Morogoro umetajwa kuwa ni kapu la uzalishaji wa mazao ya kilimo hapa nchini kuna haja ya viongozi wa ngazi zote kutoa machango wao katika kuhakikisha kuwa Lugaluga inakuwa mfano bora wa ushirika mkoani Morogoro na kwa Taifa. Jambo la msingi ni kusimamia na kuona kuwa wanachama wake wanapata mikopo itakayowawezesha katika uzalishaji kwa kununua pembejeo za kilimo, kutayarisha mashamba na kupata teknolojia za kisasa za kilimo.

Vyombo husika vitayarishe mipango na kuitekeleza katika kuboresha miundo mbinu ya shambani na hasa barabara. Hili ni tatizo kubwa lilojitokeza wakati wa kutayarisha mashamba kwa msimu wa mwaka 2007/08.

No comments: